Tuesday 27 August 2013

Mabadiliko CCM

Na HAMIS SHIMYE, DODOMA
HALMASHAURI Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM, imefanya mabadiliko makubwa kwa lengo la kuimarisha safu ya uongozi kwa kuteua makatibu wapya 28.
Katika orodha hiyo, makatibu 25 watapangiwa kazi wilayani na watatu wameteuliwa kujaza nafasi za mikoa zilizoachwa wazi.
Mabadiliko hayo pia yatawakumba makatibu wakuu wa jumuia za Chama, ambapo tayari aliyekuwa Kaimu Katibu wa CCM Mkoa wa Morogoro, Sixtus Mapunda, amependekezwa kuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM).
Kwa sasa nafasi hiyo inashikiliwa na Martine Shigela, ambaye alichukua nafasi hiyo kutoka kwa Francis Issack.
Wengine waliopendekezwa kuchukua nafasi za ukatibu mkuu kwenye jumuia hizo ni Amina Makilagi (UWT), ambaye anashika nafasi hiyo kwa sasa na Seif Shabani Mohamed atakayemrithi Khamis Suleiman Dadi.
Pamoja na mabadiliko hayo, NEC pia imemvua uanachama Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi Mansoor Yussuf Himid (Kiembesamaki -CCM), kutokana na kukisaliti na kuikana Ilani ya uchaguzi.
Katibu wa NEC ya CCM, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye alisema NEC imefanya mabadiliko hayo kwa lengo la kuongeza nguvu na kukiwezesha Chama kuendelea kushika dola.
Alisema baada ya uteuzi huo makatibu hao watapangiwa kazi katika wilaya mbalimbali hapo baadaye.
Aliwataja makatibu wa mikoa walioteuliwa kuwa ni pamoja na Mary Maziku, Kassim Mabrouk Mbaraka na Romuli Rojas John.
Kwa upande wa makatibu wa wilaya walioteuliwa ni Ashura Amanzi, Rukia Said Mkindu, Elias Mpanda, Jonathan Mabihya, Mulla Othaman Zuber, Jumanne Kapinga, Ali Hajai Makame, Jacob Makune, Juma Mpeli na Hawa Nanganjau.
Wengine ni Abdulrahman Shake, Subira Mohamwed Ameir, Abdalla Shaban Kazwika, Juma Bakar Nachembe, Josephat Ndulango, Rajab Uhonde, Abeid Maila, Mohamed Lawa, Mariam Sangito Kaaya na Bakar Lwasa Mfaume.
Kwa mujibu wa Nape wengine ni Julius Peter, Jumanne Kitundu Mginga, Mathias Nyombi, Agness Msuya na Mohamed Hassan Moyo.
Kuhusu makatibu wakuu wa jumuia za Chama, Nape alisema baada ya mapendekezo hayo watapelekwa kwenye mabaraza ya jumuia husika kwa ajili ya kuthibitishwa.
"Tumemaliza vizuri mkutano wetu wa Halmashauri Kuu kwa mafanikio makubwa kwani, hoja zote zilijadiliwa kwa kina na kuyapatia majibu," alisema.
Kuhusu kuvuliwa uanachama kwa Mansoor, alisema NEC imefikia hatua hiyo baada ya kujadili kwa kina tuhuma mbalimbali za mwakilishi huyo katika mkutano wake.
Alisema baada ya kupitia kwa kina tuhuma hizo, Halmashauri Kuu Taifa imebariki mapendekezo ya Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa wa Magharibi Zanzibar ya kumvua uanachama.
Alisema kufuatia hali hiyo NEC imebariki mapendekezo hayo na kwamba, kuanzia jana Mansoor si kiongozi tena wa CCM.
Nape alisema kufuatia uamuzi huo wa halmashauri Kuu kubariki kuvuliwa uanachama, mwakilishi huyo hana nafasi ya kukata rufaa sehemu yeote katika chama.
"Huu ndio uamuzi wa mwisho na mwakilishi huyo, hana nafasi tena ya kukata rufaa juu ya uamuzi huo wa NEC,'' alisema.
Akizitaja tuhuma zake, Nape alisema Mansoor alishindwa kusimamia malengo ya CCM, kutekeleza masharti ya uanachama na kushindwa kutekeleza wajibu wa mwanachama na kukiuka maadili ya viongozi. 
"Kutokana na mjadala mzito kamati Kuu imebariki mapendekezo ya Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa wa Magharibi Zanzibar ya kumvua uanachama wa CCM na kuanzia sasa si mwanachama wa CCM wala kiongozi wa CCM" alisema Nape.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru