Tuesday 20 August 2013

Tisa wajeruhiwa msafara wa Mwenge



Na Theodos Mgomba, Dodoma
WATU tisa wamejeruhiwa, akiwemo Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa, Juma Ally Simai (32), baada ya msafara wao kupata ajali katika kijiji cha Fufu, wilayani Chamwino.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Susan Kaganda, alisema jana kuwa, ajali hiyo ilitokea saa 3.30 asubuhi, wakati msafara ukitoka Chamwino kwenda wilayani Mpwapwa.
Alisema Simai amelazwa katika hospitali ya rufani ya mkoa wa Dodoma kwa matibabu.
Susan alisema baada ya msafara kufika katika kijiji hicho, moja ya gari lilifunga breki ghafla, ndipo magari manne yaliyokuwa nyuma yalipogongana.
Aliwataja majeruhi wengine waliolazwa katika hospitali hiyo kuwa, Charles Mamba (39), diwani wa Ipagala, Manispaa ya Dodoma, Dativa Kimolo (46), ambaye ni Ofisa Mifugo wa Manispaa ya Dodoma na Amina Mgeni (36), muuguzi wa kituo cha afya Makole, Manispaa ya Dodoma.
Wengine waliotibiwa na kuruhusiwa ni Jackline Magoti (39), Richard Mahelela (51), Jumanne Ngede (58), Zaituni Varinoi (43) na Gandula Chimponda (40).
Kaimu Mganga Mkuu wa hospitali hiyo, Dk. Zainab Chaula, alisema amepokea majeruhi tisa na hadi jana mchana Simai alikuwa bado amelazwa.
Alisema hali yake inaendelea vizuri na anatarajiwa kuruhusiwa endapo ataendelea hivyo.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru