Friday 9 August 2013

Umri wa kustaafu majaji wapingwa



UMRI wa miaka 70 wa kustaafu jaji mkuu na majaji wa mahakama ya juu uliopendekezwa kwenye Rasimu ya Katiba mpya umepingwa, na kupendekezwa uwe miaka 65.
Hoja hiyo ilitolewa na mjumbe wa Baraza la Katiba kutoka kata ya Maili Moja, Andrew Lugano, wakati akichangia mjadala wa Rasimu ya Katiba mjini Kibaha.
Alisema ibara ya 155 ya rasimu, imeweka miaka 70, lakini anapendekeza iwe miaka 65, kwani mtu anakuwa amezeeka na anapaswa kupumzika.
“Hata katika vitabu mbalimbali, vikiwemo vya maandiko matakatifu, umri wa kuishi duniani ni miaka 70, hivyo akistaafu miaka 65 anapata miaka mitano ya kula pensheni,” alisema.
Naye Alex Warioba, alitaka kiongozwe kifungu kwamba, miaka miwili kabla ya kustaafu wasipewe kesi ili wapate muda wa kumalizia za nyuma.
Alisema uzoefu unaonyesha kuna kesi nyingi zinachelewa kumalizika kutokana na majaji kustaafu, hivyo hukabidhiwa kwa mwingine jambo ambalo linachelewesha utoaji haki.
Ibara ya 155, kifungu cha kwanza inasema Jaji Mkuu na Naibu Jaji Mkuu watashika madaraka mpaka watakapofikisha miaka 70, isipokuwa kama watajiuzulu au kuvuliwa wadhifa kwa mujibu wa katiba.



Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru