Thursday 1 August 2013

China yakabidhi dawa za malaria za bil. 2/-


NA RACHEL KYALA.
SERIKALI ya China imeipatia Tanzania msaada wa dawa za kutibu malaria zenye gharama ya takriban sh. bilioni mbili.
Msaada huo wa dawa aina ya Artemisinin iliyogunduliwa nchini China, ulikabidhiwa jana kwa Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Hussein Mwinyi mjini Dar es Salaa
Akizungumza wakati wa kukabidhi msaada huo, Balozi wa China hapa nchini, Lu Youging, alisema kuwa, dawa hizo zinafaa kwa matumizi ya binadamu na kwamba hazina madhara.
“Sisi kama marafiki wa karibu wa Tanzania hatufurahi kuona malaria ikiendelea kuwa tatizo kwa Watanzania, hivyo tutatoa ushirikiano kadri tuwezavyo ili kutokomeza ugonjwa huo,” alisema Youging.
Balozi huyo alisema kuwa China ilikuwa miongoni mwa nchi nyingi duniani zilizokuwa zikiathiriwa kwa kiasi kikubwa na ugonjwa huo, lakini hivi sasa umetokomeza.
Akizungumza wakati akipokea msaada huo, Dk. Mwinyi alisema kuwa uhusiano katika sekta ya afya baina ya nchi hizi mbili umedumu kwa miaka mingi, ambapo China imekuwa ikileta madaktari mara kwa mara kuja kufanya kazi hapa nchini.
“Tayari imeshaleta makundi zaidi ya 24 ya matibabu kuja kufanya kazi na kwa sasa kuna madaktari zaidi ya 2,000 wanaofanya kazi katika maeneo mbalimbali nchini,” aliongeza.
Waziri huyo alisema baadhi ya misaada iliyotolewa na nchi hiyo kwa Tanzania licha ya msaada huo ni ujenzi wa hospitali ya moyo na kuchukua wataalamu wa afya wa hapa nchini kwenda kupatiwa mafunzo nchini humo.
Waziri huyo aliishukuru serikali ya China kwa msaada huo na kuongeza tangu ilipoanza kuisaidia Tanzania dawa za malaria, takwimu zinaonyesha vifo dhidi ya ugonjwa huo vimepungua kutoka asilimia 18 mwaka 2007 hadi asilimia 10 mwaka jana na maambukizi yakipungua kwa asilimia 50.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru