Wednesday 23 April 2014

Walimu watakiwa kuacha ushabiki


na mwandishi wetu, dodoma
WALIMU na watumishi wengine nchini, wameshauriwa kutoshabikia serikali tatu huku wao wakiwa na madai na wanashindwa kulipwa kutokana na serikali zilizopo hivi sasa kukosa fedha.
Mmoja wa wajumbe wa Bunge la Maalumu la Katiba, Menrad Kigola, alisema inashangaza kusikia kuwa hata kundi la baadhi ya walimu nao wanapendekeza uwepo wa muundo wa serikali tatu.
“Kila siku tunasikia walimu hao hao wakilalamikia mshahara kuwa ni mdogo waongezwe, lakini bado ndiyo hao hao wanataka serikali tatu, ambazo ni kuongeza gharama za uendeshaji,’’ alisema
Alisema wafanyakazi wengi pia wamekuwa wakilalamikia kodi kubwa wanayokatwa, lakini nao pia wamekuwa wakipendekeza muundo wa serikali tatu.
“Kumbukeni kama serikali ya tatu itapita, lazima na kodi itaongezeka, sasa hapo mmetatua matatizo au umeongeza matatizo kwa kuongeza kodi,’’ alisema Kigola.
Alisema ni muhimu sasa kwa Watanzania kuelewa kuwa serikali inayotakiwa na kupendekezwa na walio wengi ni ile ambayo itabana matumizi bila kutegemea misaada.
Naye Paulo Kimiti; alisema ni muhimu kwa Watanzania kujua ni mfumo upi ambao utawasaidia kupunguza kero zao.
Alisema ni muhimu kwa wajumbe kuhakikisha kuwa katiba inayoendelea kutungwa hivi sasa inawagusa wananchi wengi na si kwa manufaa ya wachache.
Kimiti alisema, Bunge Maalumu la Katiba ni la kihistoria na endapo wajumbe wake watayumbishwa na watu wachache watahukumiwa na wananchi.
Alilalamikia kitendo cha UKAWA kutoka ndani ya bunge na kueleza kuwa kitendo hicho ni cha uwoga.
Alisema, yeye binafsi alishaambiwa kuwa  asili ya uongozi ni mbili ikiwemo kuheshimu watu kwa maana ya waliokutuma na kuwatendea haki wananchi hao jambo ambalo UKAWA hawajalifanya.
“Nchi hii imejengwa kwa miaka mingi zaidi ya 50, lakini leo tunataka kuvunja muungano wetu kwa siku moja tu, hilo ni jambo la hatari sana kwani mengi yatatokea,’’ alisema.
Hata hivyo, mjumbe huyo ambaye ni mkongwe katika siasa, alisema tabia ya kuwakejeli waasisi wa Taifa si nzuri.
Alisema, hata kutoka nje kwa UKAWA  ni moja ya kazi ya mizimu ya waasisi hao kutokana na kuwatusi pasipo sababu na  wasipo jirekebisha katika hilo, hawawezi kurudi.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru