Friday 11 April 2014

Bilionea akufuru Maliasili

  • Ni Howard Buffet aliyetoa helkopta kwa JK
  • Amwaga Bil. 8.5/= kupambana na majangili
  • Jangili aliyeua faru, askari auawa kwa risasi
Na waandishi wetu
BILIONEA wa Marekani, Howard Buffet ameahidi kutoa zaidi ya sh. Bilioni 8.5 kusaidia harakati za serikali katika kupambana na ujangili nchini.
Sehemu ya fedha hizo zitakwenda kusaidia shughuli za uhifadhi wa wanyamapori katika hifadhi na mapori ya akiba.
Buffet, ambaye ni mtoto wa bilionea anayeshika nafasi ya pili kwa utajiri nchini Marekani, Warren Buffet, alitangaza neema hiyo jana, ambapo fedha hizo zitatumika kununua helkopta, magari ya doria, mafunzo kwa askari wa wanyamapori na kujenga mabweni katika Chuo cha Wanyamapori cha Pansiasi.
Mpango huo ni kuunga mkono hatua madhubuti zinazochukuliwa na serikali ya Rais Jakaya Kikwete kushinda vita dhidi ya ujangili. 
Akizungumza na watumishi na askari wa wanyamapori katika Chuo cha Pansiansi jijini Mwanza jana, Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, ambaye aliambatana na Buffett na ujumbe wake kutoka Marekani, alisema huo ni mkakati wa kutekeleza mpango wa kutokomeza ujangili alioutangaza Machi 13, mwaka huu.

Serikali imechukua hatua madhubuti kuongeza vitendea kazi, rasilimali watu na miundombinu muhimu kwa Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN). Tunashirikiana na wadau wa uhifadhi na jumuia za kimataifa kuhakikisha taifa linashinda vita dhidi ya ujangili,  alisema.
Alisema Buffett ni mdau mkubwa wa masuala ya uhifadhi na kwamba hatua yake ya kuunga mkono jitihada za serikali ni ushirikiano mpya baina ya Tanzania na Taasisi ya Howard G Buffett Foundation (HGBF).

Taasisi ya Buffet imetoa helkopita kwa ajili ya Pori la Akiba la Selous na kutoa mafunzo kwa marubani wane. Serikali pia imeagiza helkopita zingine, alisema Nyalandu.
Alisema taasisi hiyo pia itakodi helkopta zingine kwa ajili ya doria, ambazo zitakuwa chini ya usimamizi wa Idara ya Wanyamapori kwa kipindi cha miezi sita kusubiri mpya ambayo inaendelea kutengenezwa kiwandani.
Pia ameahidi kuboresha miundombinu katika Chuo cha Pansiansi pamoja na kuimarisha mafunzo kwa askari wanyamapori nchini.
Misaada mingine iliyotolewa na Buffet ni magari matano ya doria, kujenga mabweni sita kwa ajili ya wanafunzi, jiko la kisasa pamoja na karakana kwenye chuo hicho.
Pia itahusisha ununuzi wa mabasi mawili aina ya Scania, malori, mahema na vifaa vingine ambavyo vitatumiwa na wanafunzi wa chuo hicho, lengo likiwa ni kuboresha taaluma hiyo na kuwajengea ari ya kulinda maliasili askari wa wanyamapori.

Jangili aliyeua faru auawa
Katika hatua nyingine, Polisi mkoani Simiyu kwa kushirikiana na askari wa Idara ya Wanyamapori
katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, wamemuua jangili sugu Majadiga Makabajinga au Mashaka Sai, kwa kumchapa risasi ya mgongo.
Sai, ambaye alikuwa akisakwa kwa muda mrefu, anatuhumiwa kuwa kinara wa ujangili na aliuawa wakati akipambana na polisi alipojaribu kuwatoroka baada ya kutiwa mbaroni.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Simiyu, Charles Mkumbo, alisema Sai aliuawa juzi saa 3:00 usiku katika kijiji cha Mwasinansi wilayani Bariadi.
Alisema mtuhumiwa huyo alitiwa mbaroni na baada ya kuhojiwa alikiri kuhusika kwenye matukio mbalimbali ya ujangili pamoja na kifo cha askari wa wanyamapori.
Mbali na kuhusika kwenye matukio hayo, Sai alikuwa akiwafanyia ukatili ikiwa ni pamoja na kuwaua raia aliowahisi wanatoa taarifa zake kwa vyombo vya usalama.

Alibanwa na kukiri kuhusika na ujangili na siku nyingi tulikuwa tunamsaka. Ndiye alihusika na mauaji ya faru katika Hifadhi ya Serengeti (Mama Serengeti), alisema Kamanda Mkombo.
Hata hivyo, alisema baada ya mahojiano hayo, askari walimtaka awapeleke mahali anapohifadhi silaha, ndipo alipowapeleka katika kijiji cha Mwasinasi, ambapo awalionyesha sehemu ya kichaka.
Wakati askari wakifanya upekuzi kutoa silaha hizo, Sai alichukua mti na kumshambulia askari wa wanyamapori Christian Mlema kichwani kisha  kumpora silaha na kuanza kufyatua risasi hewani.
Polisi walianza kujibu na kufanikiwa kumpiga risasi mgongoni na kudondoka.
Katika kichaka hicho, polisi walikuta bunduki mbili SMG iliyokuwa na magazine mbili na SR moja, zote zikiwa na risasi 50 pamoja na meno ya tembo.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru