Wednesday 23 April 2014

‘Tutunge katiba tusijadilili watu’


WAJUMBE wa Bunge Maalumu la Katiba wameshauriwa kurejea katika kutunga katiba badala ya kujadili watu kwa majina yao.
Kauli hiyo ilitolewa jana na Mjumbe mmoja wapo wa Bunge Maalum la Katiba, Dk. Tulia Akson, alipokuwa akichangia rasimu ya katiba mjini hapa.
Alisema wajumbe wengi hivi sasa wameacha kujadili Katiba, wanajadili watu, jambo ambalio si lililowaleta bungeni.
“Katiba ndiyo iliyotuleta hapa, kwahiyo kama tunajadili, tujadili rasimu siyo kuchukua muda mwingi kuwajadili watu ndani ya Bunge,’’ alisema.
Alisema kitakacho kwenda kwa wananchi baada ya Bunge Maalumu kukamilisha kazi yake ni rasimu ya katiba na siyo majina ya watu.
Naye Velonica Sophu; alisema inashangaza kuona mjadala wa mchakato wa rasimu umeshikiliwa zaidi na wanasiasa kuliko wajumbe wengine wa kundi la 201.
Alisema, hivi sasa makundi makubwa wakiwemo wanasiasa, wameuteka mjadala huo na kuwafanya wajumbe wengine kushindwa kuchangia yale waliyotumwa na makundi yao.
Mjumbe huyo alisema awali, Tume hiyo ilipopita kwa wananchi kulikuwa na matatizo machache makuu lakini kila kukicha yanaongezeka.
“Malalamiko ya wananchi walio wengi kwanza tulisikia ni kupunguza madaraka kwa serikali, halafu tukaja hapa tukasikia masuala la muungano na sasa tunasikia masuala ya serikali tatu, sasa hata yale tuliyotumwa na wananchi wetu hayajasikilizwa,’’
Mjumbe huyo anayewakilisha kundi la wakulima, alisema wao wametumwa kuwasilisha masuala ya wakulima katika katiba ikiwemo masuala ya ardhi.
“Wakulima wetu kule wanalalamikia masuala ya ardhi, wafugaji na watu wengine, lakini hapa tunasikia masuala mbalimbali ya serikali tatu, muungano hakuna, masuala ya wakulima hebu na haya yasikilizwe basi,’’ alisema.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru