Wednesday 23 April 2014

Vigogo nishati na madini matatani


Na Latifa Ganzel, Morogoro
WATENDAJI na watumishi wa Wizara ya Nishati na Madini, waliojilimbikizia vitalu vya madini wako kwenye wakati mgumu kutokana na serikali kuagiza wachunguzwe.
Pia, imeagiza wachukuliwe hatua za kisheria ikiwa ni pamoja na kufikishwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU).


Agizo hilo lilitolewa jana na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo alipokuwa akifungua  Baraza la Wafanyakazi wa wizara hiyo mjini Morogoro, ambapo alisema baadhi ya watumishi wanadaiwa kujilimbikizia vitalu.
Alisema tatizo hilo limekuwa sugu kwa watumishi wa wizara yake huku baadhi wakitumia majina tofauti kwa lengo la kuficha ukweli, jambo ambalo limekuwa likiwakwaza wachimbaji wadogo na watanzania kwa ujumla.
Alisema baadhi ya watumishi wamejilimbikizia maeneo makubwa ya vitalu vya madini na kuagiza waanze kuchukuliwa hatua ili kupunguza malalamiko ya wananchi.
Pia, aliagiza suala la upatikanaji wa leseni za uchimbaji kutolewa kwa haraka na zile zilizoombwa bila kufuata utaratibu, zichunguzwe kisha zifutwe haraka.
Profesa Muhongo alisema kwa sasa sekta ya madini imekuwa kwa asilimia 15, ambazo hajaridhika nazo na kutaka hatua za haraka zichukuliwe ili kufikia malengo waliyojiwekea.
Naye Kamishna wa Madini, Mhandisi Paul Masanja alisema wameanza kuchambua maombi yote ya vitalu na ifikapo Julai Mosi, mwaka huu, utoaji wa leseni utakuwa umekamilika.
Alisema uchambuzi huo utasaidia kuwabaini watumishi wote waliokwapua maeneo makubwa ya vitalu vya madini na kwamba, watanyang’anywa bila kujali wadhifa wao.

Hata hivyo, alisema leseni 184 zimefutwa, 80 zikiwa zimesitishwa na leseni 150 za utafutaji madini zilifutwa na hii ni kutokana na agizo la  bunge la kuitaka wizara kufanya marekebisho.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru