Thursday 17 April 2014

Profesa Kayumbo: Lipumba amekosa hekima


NA HAMIS SHIMYE
ALIYEKUWA Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Hosea Kayumbo amesema kitendo kilichofanywa na Profesa Ibrahimu Lipumba kuwahamisha wajumbe wa bunge maalumu kutoka ndani ya bunge ni ukosefu wa hekima na uadilifu.
Pia amesema kitendo cha Profesa huyo kuwafananisha wabunge wa bunge hilo, kutoka Chama Cha Mapinduzi ni waauji wa Intarahamwe ni jambo baya linalopaswa kukemewa na siyo siasa.
Profesa Kayumbo aliyasema hayo jana katika mahojiano na Uhuru, ambapo alisema Profesa Lipumba anapaswa kuzungumza na wenzake na kurudi ndani ya bunge kwa kuwa wanachofanya si demokrasia.
“Imenisikitisha kwa mtu kama Profesa Lipumba kukosa uadilifu na hekima na hata kuwafananisha wabunge kutoka CCM ni wauaji wa Rwanda. Akiwa kama mnyamwezi wa Tabora, alipaswa kuvumilia na hata kutambua kauli yake ina madhara gani kwa jamii,’’ alisema.
Profesa Kayumbo alisema wanasiasa hawagombani bali wanatofautiana kihoja  na kinachofanywa na wajumbe hao kutoka Umoja wa Kutetea Katiba ya Wananchi (UKAWA) si kitendo cha kiungwana.
Alisema kususua bunge ni kuonyesha kutokomaa kisiasa na ‘poor judgment of events’. Alisema pamoja na kuonyesha uwezo wa kutoa hoja kipindi cha awali, wanapaswa kurudi bungeni.
“Waache hila na warudi bungeni kutetea hoja zao,ambazo awali walikuwa wanazitoa kuhusiana na mchakato wa upatikanaji wa katiba mpya kama inavyotarajiwa na wananchi,’’alisema.
Profesa Kayumbo alisema kinachofanywa na watu wa UKAWA ni jambo baya na linalotoa taswira mfu katika kujenga mtazamo wa hoja juu ya mchakato mzima wa Katiba Mpya,ambayo watanzania wanaitegemea.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru