Friday 11 April 2014

Moto wateketeza bweni la wanafunzi Dar

NA JESSICA KILEO

MOTO umezuka ghafla kwenye bweni la shule ya sekondari ya Father  Andrew  Memorial na kuliteketeza lote pamoja na mali zilizokuwemo ndani yake.

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo, Kamanda wa Polisi mkoa wa Kinondoni, Camilius Wambura alisema tukio hilo lilitokea juzi saa 6.00 usiku katika shule hiyo iliyoko katika
maeneo ya Salasala IPTL, Kinondoni, Dar es Salaam.

Wambura alisema moto huo ulizuka ghafla kwenye bweni la wavulana, mali ya shule hiyo na kulitekeleza lote, ikiwa ni pamoja kuharibu mali zilizokuwamo ndani yake.

Alisema hakuna madhara yoyote yaliyotokea kwa binadamu na kwamba tukio hilo lilitokea wakati wanafunzi wakiwa likizo.

Kamanda Wambura alisema chanzo cha moto huo bado hakijafahamika na upelelezi unaendelea.

Wakati huohuo, watu sita wamekamatwa katika maeneo ya Kariakoo wakiwa na dawa za kulevya pamoja na pombe haramu aina ya gongo.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Ilala, Marietha Minangi alisema jana kuwa watu hao walikamatwa juzi saa 12.00 jioni maeneo ya Livingstone, Kariakoo.

Marietha alisema kukamatwa kwa watu hao kumetokana na msako maalumu uliofanywa na jeshi hilo.

Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Ashrafu Bashiri (32), Japhet Komba (40) na wenzao wanne.

Alivitaja vitu walivyokamatwa navyo kuwa ni bunda moja la mirungi pamoja na lita mbili za pombe haramu aina ya gongo.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru