Wednesday 23 April 2014

Bulembo amshukia Jaji Warioba


NA THEODOS MGOMBA, DODOMA
MJUMBE wa Bunge Maalumu la Katiba, Abdalah Bulembo, jana alimshukia aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya marekebisho ya Katiba, Jaji Joseph Warioba, kuwa hana nia nzuri na taifa kutokana na kusimamia mapendekezo ya kutaka nchi iwe na serikali tatu.


Akichangia bungeni jana katika mjadala wa Rasimu, Bulembo alisema hali hiyo imejionyesha kutokana na shinikizo lake, la kutaka serikali tatu kwa madai kuwa ni mapendekezo ya wananchi walio wengi.
“Dhambi hii ya kutaka uwepo wa serikali tatu au shirikisho ni ya kutaka kuuwa muungano na haita mmaliza Maalim Seif Hamadi tu, bali hata baadhi ya viongozi,’’ alisema Bulembo.
Alisema kama kuna watu wanafikiria serikali ya tatu ndiyo moja ya njia ya waarabu kurudi Zanzibar, hiyo haitawezekana chini ya Serikali ya CCM.
“Mimi imenishangaza kuona Waziri wa Sheria wa Zanzibar, naye anainuka na kutaka serikali ya shirikisho je, kama siyo muungano ambao umeleta serikali ya maridhiano angepata wapi uwaziri,” alihoji Bulembo.
Mjumbe huyo, alisema Zanzibar kudai kuvunjika kwa muungano ili wapate serikali kamili sasa haitawezekana, na muungano utaimarishwa zaidi ya sasa.
“Mheshimiwa Makamu Mwenyekiti, sisi tunasema tukimaliza hapa, mimi nitaanza safari ya kwenda Lindi, Mtwara na hata Njombe, kwenye majukwaa kuwaeleza wananchi nini wao wamefanya,’’ alisema.
Aidha, alisema ni muhimu kwa sasa Bunge likaweka sheria juu ya watu wanaowasema viongozi waasisi walioliunda taifa.
Alisema kuanzia sasa ni vyema watu wa aina hiyo wakashitakiwa au kutolewa ndani ya Bunge na askari wa bunge.

Komba: Serikali tatu ni uasi
Naye Kapteni mstaafu John Komba, alisema kitendo cha mapendekezo ya Tume ya Jaji Warioba kupendekeza serikali tatu, ni sawa na binadamu wa kwanza waliomuasi Mungu.
“Mimi nitakuwa wa mwisho kukubaliana na pendekezo hilo na kama litapita, nitaingia msituni kwenda kupigania serikali mbili,’’ alisema Komba.
Alisema pamoja na binadamu hao wa kwanza kupewa adidu za rejea, bado walimuasi Mungu na kisha kufukuzwa katika bustani ya Edeni
“Alichofanya Warioba ni sawa na binadamu hawa wa kwanza, kwani walipewa adidu za rejea lakini wao wamekuja na kitu chao, kwani awali Rais Kikwete aliwapa adidu kuwa pamoja na mambo mengine, suala la muungano lisiguswe, lakini wao wameligusa.
“Katika Tume ile kulikuwa na watu muhimu sana ambao walikuwa karibu sana na Hayati Mwalimu Julius Nyerere na walikuwa wakinywa chai na mikate pamoja na hata mambo mengine huwezi kuyapata toka kwa Nyerere bila ya wao,’’ alisema.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru