Thursday 17 April 2014

Kinana amshangaa Lipumba


Na Suleiman Jongo, Mpanda
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimemshangaa Mjumbe wa Bunge Maalum la Katiba, Profesa Ibrahim Lipumba kutokana na madai yake kuwa CCM imekuwa ikitumia lugha za matusi katika kutetea hoja mbalimbali ndani ya bunge hilo.


Akizungumza kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika mjini Mpanda jana, Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana alisema wajumbe wa Bunge hilo wanaotokana na CCM si chanzo cha matusi bali wapinzani ndio wenye kuanzisha matusi bungeni.
“Prefesa Lipumba amewashutumu wajumbe wa CCM akidai wamekuwa wakitumia lugha za matusi. Namshangaa kwa kuangalia upande mmoja wakati wapinzani ndio walioanza lugha chafu, sasa lawama za nini,” alisema.
Kinana aliwataka Watanzania kutoghiribiwa na vitendo vitendo vya wajumbe wa bunge hilo, hususan wanaoshinikiza mfumo wa serikali tatu kwa kuwa si ajenda itakayowaletea maendeleo ya moja kwa moja.
Alisema jambo la muhimu kwa wananchi kufanya kazi kwa bidii kwa kuwa ndio kitu pekee kitakachowaletea maendeleo wakiwa kwenye mfumo wa katiba yoyote.
“Msisikilize propaganda za watu waliokata tamaa, wananchi fanyeni kazi ndiyo itakayokuwekeni kwenye maisha mazuri, katiba mpya haiwezi kukuleteeni chakula cha kila siku. Hata ikipitishwa leo, maisha yatabaki kuwa ni yale yale,” alisema.
Katika hatua nyingine, Kinana aliwataka wanachama wa CCM kuwa wa kwanza katika kuikosoa serikali badala ya kusubiri wapinzani kwa kuwa sio wenye ilani ya uchaguzi inayotekelezwa.
Aidha aliitaka serikali kuondoa urasimu wa kodi kama njia ya kuimarisha uchumi wa wananchi.
“Maisha ya Watanzania hayataweza kubadilika na kupambana na umaskini endapo tutaendelea kuwa na vikwazo vingi vya kodi,” alisema.
Naye Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alisema kutoka ndani ya bunge kulikofanywa na wajumbe wa upinzani, kunatokana na kulipwa posho wiki nzima za vikao vya Bunge hilo.
“Kama UKAWA wana msimamo wasirudi tena bungeni. Endapo watarudi, ni wazi Watanzania tutawaona wanafanya mchezo wa kitoto,” alisema.
Juzi wajumbe wanaounda UKAWA walisusia na kutoka bungeni kwa madai ya kuchoshwa na lugha za matusi zinazotumika ndani ya Bunge hilo.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru