Friday 11 April 2014

Viongozi wa dini wawajia juu watendaji wa serikali


NA SULEIMAN JONGO, KASULU

VIONGOZI wa madhehemu mbalimbali ya dini wilayani Kasulu mkoani Kigoma, wamewajia juu watendaji wa serikali kwa kuendekeza rushwa, hali inayosababisha kukosekana kwa haki miongoni mwa jamii.

Wamemuomba Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana kuisimamia serikali katika vita dhidi ya tatizo hilo ili kutoa fursa kwa wananchi kupata huduma bila mizengwe.

Akizungumza katika mkutano kati ya Kinana na viongozi wa dini uliofanyika wilayani humo, Mchungaji wa Kanisa la Assembly of God (EAGT) wilayani humo, Edward Bakana alisema rushwa imesababisha hali ya upatikanaji huduma kuwa ya hovyo ikilinganshwa na malengo ya serikali.

“Rushwa katika Kasulu yetu imekuwa mbaya, kitu ambacho hakimpendezi Mungu.
Ili mwananchi apate huduma, lazima atoe rushwa. Hali hii haipaswi kufumbiwa macho," alisema.

Alisema rushwa imesababisha baadhi ya wafanyabiashara wakubwa wilayani humo kupitishia bidhaa zao katika nchi za Kenya, Rwanda na Burundi badala ya Kasulu ambayo ni rahisi zaidi.

“Kama kweli tunataka maendeleo, hali hii lazima ifanyiwe kazi kuhakikisha huduma zinapatikana kwa urahisi kisheria bila kuwepo urasimu," alisema.

Mchungaji huyo alisema anaishangaa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), kuelemewa na kutofuatilia vitendo vya rushwa vilivyoko wilayani humo.

Naye Mwenyekiti wa Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) wilaya ya Kasulu, Sheikh Kabaka Athuman alimuomba Kinana kuitazama polisi wilayani humo, kutokana na kukithiri kwa madai ya askari wake kuongoza kwa kuomba na kupokea rushwa.

“Sisi viongozi wa dini tunaomba tatizo hili la rushwa lishughulikiwe kwa kuwa ni miongoni mwa mambo makubwa yanayosababisha wananchi kuichukia serikali, ambayo imekuwa ikijitahidi kutafuta huduma mbalimbali na kuwaletea wananchi, hasa huduma za afya bure kwa wajawazito na watoto walio chini ya umri wa miaka mitano," alisema.

Akizungumza kuhusu hoja ziliziotolewa, Kinana aliwataka viongozi hao kuhakikisha wanashirikiana na serikali ili kutatua changamoto za wananchi na kuepusha mgawanyiko wa kiimani ambao ni hatari kuliko kitu chochote.

Kuhusu tuhuma za rushwa kwa taasisi za serikali, Kinana alimuagiza Mkuu wa Wilaya hiyo, Dani Makanga kuzifanyia kazi na kuondoa kero hiyo.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru