Tuesday 8 April 2014

Tanzania yauza nje mifugo 7,422


NA MWANDISHI WETU, MISUNGWI

TANZANIA iliuza mifugo 7,422 nje ya nchi na kuingiza kiasi cha zaidi ya sh. bilioni 3.8 huku mingine milioni 1.7 ikiuzwa kwenye minada ya ndani na kuwaingizia wafugaji zaidi ya sh. bilioni 775.
Waziri wa Mifugo na Maendeleo ya Uvuvi, Dk. Titus Kamani amesema mauzo hayo ni ya kipindi cha miaka miwili iliyopita, hivyo sekta ya mifugo ikiendeshwa kibiashara, itachangia kwa kiasi kikubwa zaidi pato la taifa na kuwapa maisha bora wananchi.
Alisema hayo jana wakati akifungua mnada wa Upili uliopo katika Kijiji cha Nyamatala maarufu Ng'ombe, wilayani Misungwi, Mwanza.
Alisema kwa kipindi hicho kutoka mwaka 2011/2012, ng'ombe 3,362, kondoo na mbuzi wapatao 4,060 waliuzwa katika nchi za Kenya, Comoro na Falme za kiarabu na kuliingizia taifa sh. bilioni 3.81.
Dk. Kamani alisema nyama ya ngÕombe (tani 647), mbuzi na kondoo (tani 151.8) zilizouzwa pia katika nchi za Oman na Kuwait, ziliingiza sh. 19.3 bilioni.
Alisema bishara ya mifugo nchini imekuwa ikiendeshwa bila kuzingatia taratibu zilizopo kwa mujibu wa sheria namba 17 ya mwaka 2003, sheria ya nyama ya 2008, ustawi wa wanyama namba 19 ya 2008, sheria ya utambuzi na usajili na ufuatiliaji mifugo, hali ambayo imeleta athari nyingi za kibiashara.
Alizitaja athari hizo kuwa ni pamoja na magonjwa, wizi wa mifugo, uharibifu wa mazingira, usimamizi mdogo katika kutunza na uendelezaji miundombinu na matumizi yasiyoridhisha ya miundombinu.

Sekta hii ikiendeshwa kibiashara na kwa kuzingatia sheria na kanuni zake, itachangia kwa kiasi kikubwa sana pato la taifa na wananchi kwa ujumla, hivyo nawaomba wananchi hususan wafugaji na wafanyabiashara, wachangamkie fursa zilizopo ukiwemo mnada huu wa Upili, alisema Dk. Kamani.
Waziri huyo aliwaonya wananchi wenye tabia ya kuvamia maeneo ya serikali na ambao tayari wameisha ingia kwenye eneo la Mnada huo mpya, waache mara moja na kuondoka.
Awali, akitoa taarifa ya mnada huo, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Maendeleo ya Uvuvi, Dk. Yohana Budeba, alisema mnada huo wa Upili ni miongoni mwa miradi 12 iliyojengwa nchini mwaka 2012 kufuatia mipango iliyoanzishwa mwaka 1964 na kufikia mwaka 1966 walipatikana ng'ombe kwa ajili ya maziwa na kilimo (maksai),
lakini ilisimama kutokana na ukosefu wa fedha za kujenga miundombinu.
Dk. Kabisa alisema lengo la kuanzishwa kwa mnada huo ni pamoja na kuwezesha wananchi (wafugaji na wafanyabiashara wa ng'ombe) kuwa na soko zuri la kiuchumi na kuwawekea mazingira mazuri zaidi ya kibiashara.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru