Monday 27 October 2014

Aliyejilipua kwa risasi aibua mambo mazito


NA LILIAN JOEL, ARUSHA
SAKATA la Mkurugenzi wa Kampuni ya Kitalii ya DAGT, Timoth Mroki, kujiua kwa kujilipua kwa risasi, limeibua mambo mapya kutokana na kuelezwa kuwa wivu wa kimapenzi.
Habari zilizopatikana jijini hapa, zinasema kuwa Mroki (36), alikuwa na vimada wawili ambao ni wake za watu na kuwa kabla ya kujilipua kwa risasi na kupoteza maisha, alitoa taarifa kwa wanawake hao (majina yanahifadhiwa).
Imeelezwa kuwa Mroki alikuwa akitoka na wanawake hao kila mmoja kwa muda wake, lakini baadaye siri hiyo ilianza kuvuja na hatimaye vimada kufahamiana, ikiwa ni pamoja na mkewe kuanza kupenyezewa taarifa hizo.
Mroki, ambaye pia ni Meneja wa Operesheni na Masoko wa Kampuni ya Tanzania Bush Camp, alijiua kwa kujipiga risasi Oktoba 25, mwaka huu, saa 1:00, baada ya kubaini kuwa vimada wake hao wamefahamiana.
Habari kutoka kwa mtu wa karibu zimesema kuwa, vimada hao baada ya kufahamiana, walikutana na kufanya mazungumzo kisha kupiga picha pamoja na kumrushia kupitia simu ya mkononi.
Kugundulika kwa siri hiyo, kulizusha taharuki kwa Mroki, hivyo kusababisha kuyumba kwa uhusiano baina yake na vimada hao, akiwemo mmoja ambaye pia ni mshirika wake kibiashara.
“Hawa wanawake wana siri nzito kuhusiana na kifo hiki kwa sababu kabla ya kufanya uamuzi, aliwasiliana nao…kikubwa awali walikuwa hawafahamiani ila baadaye walikutana na kuungana kuwa kitu kimoja.
“Haifahamiki ni kwa vipi walijenga urafiki, ila watu wa karibu wanasema walijipanga kumkomoa ili afilisike kwa kuwa kila mmoja alikuwa na malengo yake,” alisema mtoa habari wetu.
Kuungana kwa wanawake hao kumlichanganya Mroki, ambaye tayari uhusiano wake nyumbani pia ulianza kuwa tete baada ya mkewe kuhisi kuna mambo yanafanyika kinyume cha utaratibu.
Hata hivyo, habari zaidi zinasema kuwa miongoni mwa wanawake hao, yupo aliyejenga uswahiba na mke wa marehemu huku uhusiano wa kimapenzi ukifichwa chini ya mwamvuli wa biashara.
Chanzo chetu kimesema kuwa, kutokana na ukaribu huo, familia hizo zimekuwa na kawaida ya kutembeleana, ikiwa ni pamoja na watoto kukaa kwa siku kadhaa nyumbani kwa kimada mmoja.
Imeelezwa kuwa kutokana na kugundulika kwa siri hiyo, Mroki alichukua uamuzi wa kujimaliza ili kukwepa aibu mbele ya familia.
“Kugonga gari si sababu ya Mroki kujiua, ni kutokana na kutingwa na mambo mengi kichwani, hasa baada ya siri ya kimapenzi kuanza kubainika,” aliongeza mmoja wa rafiki wa marehemu.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas, alisema Mroki alijiua kwa kujipiga risasi kifuani kwa kutumia bastola aina ya KEL –TEC yenye namba HCB21.
Katika taarifa yake, Kamanda Sabas alisema kabla ya tukio hilo, Mroki alikuwa na gari namba T222CMX, aina ya Isuzu Double Cabin, iliyokuwa ikitokea Mbauda kwenda katikati ya jiji.
Hata hivyo, taarifa hiyo iliongeza kuwa kutokana na msongamano wa magari, Mroki alitanua barabara kukwepa foleni huku akiwa katika mwendo kasi.
Alipofika maeneo ya Shams, aligongana na gari la mizigo, mali ya Kampuni ya Gupta, lenye namba T548 BRL.
Taarifa ilisema pamoja na kusababisha ajali hiyo, Mroki aliendelea na safari yake ndipo madereva wa bodaboda walipoamua kumfukuza na kumkamata eneo la kona ya Nairobi Ngarenaro.
Mroki aliporejea eneo la tukio na kuulizwa sababu za kusababisha ajali na kuendelea na safari, alitoa bastola na kufyatua risasi mbili hewani na ya tatu kumpiga kifuani.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru