Monday 27 October 2014

Manufaa zaidi ziara ya JK China


NA MWANDISHI MAALUM
SERIKALI na taasisi mbili kubwa za kimataifa zimetiliana saini hati ya makubaliano (MOU) ya kuendeleza kwa pamoja Eneo la Kiuchumi la Bagamoyo.
Katika uendelezaji huo, pia itajengwa bandari kubwa ya Bagamoyo ambayo inatarajiwa kutoa mchango mkubwa kwa uchumi wa Tanzania.
Pande hizo tatu ambazo ni pamoja na Kampuni ya Uendeshaji Bandari ya China Merchant Holding International (CMHI) ya Jamhuri ya Watu wa China na Mfuko wa Uwekezaji wa Oman, zimetilia saini hati hiyo kwenye sherehe iliyofanyika katika Hoteli ya Hilton Shenzhen Shekou Nahai,  Shenzhen, Kusini mwa China.
Rais Jakaya Kikwete, ambaye alitembelea Jimbo la Guang Dong ambako liko Eneo la Uwekezaji wa Kiuchumi la Shenzhen, alishuhudia utiaji saini huo ambao kwa upande wa Tanzania saini ilitiwa  na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dk. Servicus Likwelile.
Chini ya hati hiyo, ujenzi wa Eneo la Uwekezaji la Bagamoyo utaanza Julai Mosi, mwakani. 
Kabla ya sherehe hiyo ya kutiliana saini hati ya makubaliano, Rais Kikwete alitembelea eneo la Makontena la Bandari ya Shenzhen, ambako alionyeshwa vifaa vya kisasa vya kupakia na kupakulia makontena. Kazi hiyo inafanywa na  CMHI ambayo ina uzoefu wa miaka 140 wa uendeshaji wa bandari.
Akizungumza katika sherehe hiyo, Rais Kikwete alisema kuwa serikali yake imedhamiria kuhakikisha mradi huo wa mamilioni ya fedha wa Bangamoyo unaanza.
 “Tutafanya lolote linalowezekana kuhakikisha kuwa mradi huu unaanza kwa sababu utaleta neema kubwa ya kiuchumi kwa nchi nzima,” alisema.
Naye Mwenyekiti wa CMHI, Li Jianhong, ameitaka serikali kuangalia uwezekano wa kumaliza vikwazo vyote ambavyo vimechelewesha kuanzishwa kwa mradi huo ili uweze kuanza Julai Mosi, mwakani, kama ilivyokubaliwa.
Mapema jana, akiwa Shenzhen, Rais Kikwete alitembelea makao makuu ya kampuni ya Teknolojia ya Mawasiliano ya Hauwei  inayoajiri maelfu ya watu duniani, ikiwemo Tanzania na kutengeneza mamilioni ya faida.
Rais pia alikutana na kufanya mazungumzo na viongozi wa Manispaa ya Shenzhen ambayo yalifanyika kwenye hoteli ambako alifikia ya  Shenzhen Wazhou Guest Hotel ambayo ni mali ya Serikali ya China.
Pia alitembelea makao makuu ya kampuni ya Teknolojia ya Mawasiliano ya ZTE iliyoko Shenzhen, ambayo inaendesha shughuli zake Tanzania na inaajiri wafanyakazi 60,000 dunia nzima.


Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru