Sunday 26 October 2014

Tapeli latiwa mbaroni Mbeya


Innocent Ng’oko, Mbeya
MAKACHERO wa Jeshi la Polisi Nchini, wamemtia mbaroni mmiliki wa Kampuni ya KEAR Computer Training, Uttu Kingwande, kwa tuhuma za utapeli.
Kingwande anadaiwa  kuwatapeli wanafunzi lukuki waliokuwa wakipata mafunzo ya kompyuta katika kituo chake alichokuwa amekifungua katika Shule ya Sekondari ya Mbeya.
Inadaiwa kuwa kituo hicho hakikuwa kimesajiliwa na hivyo alikuwa akijipatia pesa kiujacha ujanja.
Mtuhumiwa huyo alikuwa akitafutwa kwa zaidi ya miezi mitatu sasa, ambapo taarifa za kiuchunguzi zinaeleza kuwa alitiwa mbaroni akiwa mafichoni wilayani  Handeni, katika mkoa waTanga.
Habari za kipolisi zinasema baada ya kutiwa mbaroni, mtuhumiwa  alisafirishwa hadi Mbeya akiwa chini ya ulinzi.
Inadaiwa kuwa kituo alichokuwa akikiendesha hakikuwa na usajili unaotambulika, hivyo wanafunzi waliokuwa wakisoma walijikuta wakikosa ajira na vyeti vyao kutotambulika popote.
Hadi jana, baadhi ya  wanafunzi waliopatwa na msukosuko  wanadai hawajarudishiwa pesa zao za ada tangu mmiliki huyo akimbie na kufunga kituo kwa miezi mitatu.
Julai mwaka huu, wanafunzi waliokuwa wakipata mafunzo kituoni hapo walielezwa kuwa mafunzo yamesitishwa kwa muda kutokana na polisi kuvamia. Kila mwanafunzi kituoni hapo alikuwa akilipa sh. 40,000.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Barakael Masaki, alikiri kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo na kusema anatarajiwa kufikishwa mahakamani.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru