Sunday 26 October 2014

MSD yaidai serikali mabilioni


NA EPSON LUHWAGO 
UHABA mkubwa wa dawa na vifaa tiba umezikumba hospitali nyingi nchini, zikiwemo za Muhimbili na Ocean Road, kutokana na serikali kudaiwa zaidi ya sh. bilioni 90 na Bohari Kuu ya Dawa, (MSD).
Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika lisilo la kiserikali linalofuatilia masuala ya afya nchini la SIKIKA, Irenei  Kiria, alisema jana jijini Dar es Salaam kuwa hali hiyo inahatarisha maisha ya wananchi kutokana na kukosa matibabu.
Irene alisema kutokana na madeni hayo, MSD imesimamisha usambazaji wa dawa katika hospitali za serikali, zikiwemo za rufani na za wilaya, hasa za Mpwapwa na Kiteto, ambazo zinadaiwa mamilioni ya shilingi. 
Alisema Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, kwa mfano, inadaiwa sh. bilioni nane, huku Hospitali ya Wilaya ya Kiteto mkoani Manyara, ikidaiwa sh. milioni 38.
Kwa mujibu wa Kiria, ongezeko la deni hilo limekuwa likiathiri ufanisi na utendaji kazi wa MSD, kwakuwa taasisi hiyo haijiendeshi kwa faida.
Alisema kutolipwa kwa fedha hizo kwa wakati kunaifanya MSD kukosa fedha za kugomboa, kuhifadhi na kusambaza dawa na vifaa kutoka mahali vinakotengenezwa na katika matawi yake. 
Kutokana na hali hiyo, alisema afya za wananchi ambao wengi wao hawana uwezo wa kugharimia matibabu, ziko shakani kwa kuwa tegemeo lao kubwa ni hospitali na vituo vya kutolea huduma za afya vilivyo chini ya serikali. 
“Nchini Tanzania, zaidi ya asilimia 80 ya wananchi hawako katika mfumo wowote wa bima za afya na inapotokea uhaba wa dawa na vifaa tiba, wananchi hawa wanakuwa ndio waathirika wakubwa zaidi,” alisema.
Pamoja na taarifa ya SIKIKA, uchunguzi uliofanywa na Uhuru katika baadhi ya hospitali za jijini Dar es Salaam,  kama Sinza Palestina na Mwananyamala, unaonyesha kuwa wagonjwa wengi wamekuwa wakiandikiwa dawa na kutakiwa wakazinunue kwenye maduka ya dawa.
Mmoja wa madaktari katika hospitali ya Sinza Palestina (jina linahifadhiwa) alikiri kuwepo kwa hali hiyo na kusema tatizo hilo limekuwepo kwa zaidi ya mwezi.
Katika hospitali ya Mwananyamala ambayo ina hadhi ya rufani katika Manispaa ya Kinondoni, baadhi ya wagonjwa walisema wanandikiwa dawa huku wakiambiwa haziko kwenye hifadhi na kutakiwa kwenda kwenye maduka yaliyoko jirani. 
Hata hivyo, sababu kubwa ya serikali kutoilipa MSD ni kutokana na ufinyu wa bajeti kwa kuwa fedha zilizopangwa kwa ajili ya afya zimetolewa kidogo kulinganisha na mahitaji. 

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru