Monday 27 October 2014

Serikali yasema hakuna mgonjwa wa ebola


NA MWANDISHI WETU
SERIKALI imekanusha kuwepo kwa ugonjwa wa ebola nchini, huku ikithibitisha kuwa mtu aliyedhaniwa kuwa na ugonjwa huo, anasumbuliwa na malaria.
Pia, wanafamilia wa karibu wa mgonjwa huyo wamechunguzwa na kuonekana  hawana dalili za ugonjwa huo au magonjwa jamii ya ebola, kama dengue na chikungunya.
Kauli hiyo ya serikali imetolewa baada ya sampuli ya damu iliyochukuliwa kutoka kwa mgonjwa huyo na kufanyiwa uchunguzi wa kimaabara, kuonyesha kuwa alikuwa akisumbuliwa na malaria. 
Kwa mujibu wa tamko lililotolewa na serikali jana na Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Donan Mmbando, baada ya kupatikana kwa taarifa ya kuwepo kwa mtu wenye dalili za ebola, serikali ililazimika kumfanyia uchunguzi wa kina mgonjwa huyo.
Taarifa hiyo ilieleza kuwa mgonjwa huyo, ambaye ni mkazi wa Dar es salaam, eneo la Kimara, alifika mkoani Kilimanjaro, Oktoba 20, mwaka huu, katika kijiji cha Kirua kwa ajili ya kusalimia ndugu.
Baada ya kufika mkoani hapo, alifikishwa katika Kituo cha Afya cha Shirimatunda, akisumbuliwa na maumivu ya misuli, kichwa, maumivu ya koo na kupoteza hamu ya kula.  
Taarifa za mgonjwa huyo zilionyesha kuwa kikazi ni mtaalamu wa kupima ardhi (Land Surveyor) na katika siku za hivi karibuni, alikwenda nchini Senegal kwa kazi za mkataba na kurejea nchini mwezi huu.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru