Monday 27 October 2014

Balozi Sefue atema cheche


NA WAANDISHI WETU, DODOMA
SERIKALI imewataka viongozi waandamizi wanaoendelea kutumia risiti za kuandikwa kwa mikono katika makusanyo ya serikali kuachia ngazi kwa kuwa wameshindwa kudhibiti mapato ya serikali.
Kauli hiyo ilitolewa jana na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue, alipokuwa akifungua mkutano wa faragha wa mwaka wa makatibu wakuu, manaibu na makatibu tawala wa mikoa.
Sefue alisema mfumo ya kukusanya mapato kwa kutumia risiti zilizoandikwa kwa mikono unasababisha uvujaji mkubwa wa mapato ya serikali.
Alisema katika sehemu nyingi ambazo wameacha kutumia mfumo huo na kutumia mfumo wa kieletroniki kumekuwa na mafaniko makubwa katika ukusanyaji wa mapato.
‘’Katika Hospitali ya Tumbi mapato yaliongezeka kutoka wastani wa sh. 380,000 hadi sh. milioni tatu kwa mwezi, baada ya kutumia mfumo wa kiletroniki,’’ alisema.
Alisema ni lazima kusimamia mifumo madhubuti ya ufuatiliaji na tathimini kwa upande mmoja, mfumo wa udhibiti wa ndani katika masuala ya fedha na rasilimali nyingine.
‘’Msiwe waoga kuchukua hatua za kinidhamu au kisheria kwa wale wanaochafua sura na sifa ya utumishi wa umma.
“Ukishindwa kufanya hivyo ama wewe mwenyewe ni tatizo au hukufaa kupewa mamlaka ya nidhamu yanayoambatana na cheo ulichopewa,’’ alisisitiza.
Sefue alisema kumekuwa na upungufu katika ripoti za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali na mengine yanajirudia mwaka hadi mwaka.
Alisema katika hilo inaonyesha kutokuwa na dhamira ya ukweli katika kumaliza hoja za mkaguzi au mifumo ya udhibiti wa ndani kuwa hafifu.
‘’Sasa tunajua tatizo ni nini. Kinachotakiwa ni dhamira ya kweli miongoni mwetu tuliopo hapa na kusema sasa basi na wale watakaoshindwa kusema itabidi watupishe,‘’ alisema.
Katibu huyo alitolea mfano udanganyifu mkubwa uliogunduliwa na Mkaguzi Mkuu wa Ndani alipohakiki madai ya walimu tangu wa elimu ya msingi hadi wa vyuo vikuu na kusema udanganyifu wa aina hiyo lazima ukomeshwe.
Alisema pia mradi hati punguzo kwenye vyandarua vilivyotiwa dawa ambao ulikuwa ukiokoa maisha ya kina mama na watoto wachanga, umesitishwa na wahisani kutokana na wizi mkubwa.
“Ni hapa juzi tu nimeambia asilimia 40 ya dawa kutoka Bohari Kuu ya Dawa (MSD) zinaibwa katikati zikisafirishwa kutoka MSD hadi kufika kwa wananchi. Wizi wa aina hii lazima ukome na wahusika washitakiwe ili liwe fundisho kwa wengine,’’ alisema.
Katibu Mkuu aliwataka makatibu wakuu hao kutekeleza vyema na kwa moyo thabiti majukumu yao na kutumia mkutano huo kutafakari na kujitathimini kisha kuazimia kuwa chachu ya kweli ya maendeleo. 

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru