Monday 27 October 2014

Bunge latishwa na madudu Ranchi ya Ruvu


NA KHADIJA MUSSA
MSAJILI wa Hazina kwa kushirikiana na Wizara ya Maendeleo ya Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, wametakiwa kupitia upya ripoti ya ukaguzi ya Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) na kuchukua uamuzi ndani ya wiki tatu.
Pia Bodi ya NARCO imeagizwa kufanya tathmini iwapo menejimenti ya NARCO na ya Ranchi ya Ruvu kama zinastahili kuendelea na kazi zao na kutoa majibu katika kipindi cha wiki tatu.
Msajili ya Hazina ametakiwa kutathmini na kubaini kama Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya NARCO bado anastahili kuendelea kuwemo katika nafasi hiyo.
Maagizo hayo yalitolewa jana Dar es Salaam na Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudunu ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC), Deo Filikunjombe, baada ya kamati kutoridhishwa na utendaji wa kampuni hiyo.
Mbali na maagizo hayo, pia Filikunjombe alisema kamati yake haiwezi kukubali ombi la kampuni hiyo la kutaka serikali iwape sh. bilioni 17 kwa ajili ya kuongeza mtaji wake kwa kuwa utendaji wake hauridhishi.
Alisema kampuni hakuna sababu ya serikali kutoa fedha za walipakodi kwa ajili ya kampuni hiyo ambayo inajiendesha kwa hasara na katika kipindi cha miezi mitatu walipotea ng’ombe 376 katika ranchi moja ya Ruvu.
Pia alisema katika baadhi ya ranchi kuna watendaji ambao hawajui KKK (kusoma, kuandika na kuhesabu) na kuna taarifa zinaonyesha kuwa kwa miezi mitatu mfululizo, wachungaji wanapewa ng’ombe na hawahesabiwi wakati wa kutoka kwenda machungani na hata wa kurudi.
Aliongeza kuwa baadhi ya taarifa zao zinaonyesha kuwa asubuhi wametoka ng’ombe 300 na jioni wamerudi 400, huku baadhi ya vitabu takwimu zake si sahihi kwa kuwa zimefutwafutwa, jambo ambalo linashangaza.
Naye Dk. Hadji Mponda, mjumbe wa kamati hiyo, alisema licha ya NARCO kudai kuwa na mfumo wa kuandika idadi ya ng’ombe wanaotoka na kurudi machungani, imebainika mfumo huo si sahihi na ndiyo sababu kunakuwa na upotevu na wanazidi kupungua mwaka hadi mwaka badala ya kuongezeka.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya NARCO, Salum Shamte alisema anasikitikika na hatua hiyo kwa sababu athari yake si ndogo kwa kuwa kama suala la wizi hata wao haliwafurahishi na hatua zilichukuliwa na vyombo husika vinaendelea na uchunguzi.
Filikunjombe alisema wanatambua mchango wa shirika hilo lakini kwa sasa hawastahili kupewe hata shilingi moja kutoka kwa walipakodi kutokana na menejimenti waliyo nayo.
Katika hatua nyingine, Filikunjombe aliuliza kuhusu Machinjio ya Ruvu ambayo serikali ilitoa zaidi ya sh. bilioni tisa na hayajakamilika hadi sasa. Hata hivyo, Shamte alisema walipokea sh. bilioni 5.6 tu.
Filikunjombe alisema kamati ilifanya ziara katika machinjio hayo na kilichoonekana hakilingani ya kiasi hicho cha fedha na kusisitiza tena kuwa hakuna haja ya kampuni hiyo kupewa fedha.
“Nasikia uchungu. Ni wizi ujangili, tuko katika matatizo wengine wanafanya wizi. Tatizo ranchi hazina uzio na watu wanaingia na kutoka,” alisema Shamte.
Kuhusu ujenzi wa machinjio ya Ruvu, Shamte  alisema waliamua kusitisha baada ya mkandarasi waliyeingia naye mkataba kujenga chini ya kiwango na sasa wako katika mchakato kutafuta mkandarasi mwingine hivyo yatakamilika mwishoni mwa mwaka ujao.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru