Friday 24 October 2014

Walimu wagomea mafunzo wakidai posho


Walimu wagomea mafunzo wakidai posho 
NA CHIBURA MAKORONGO, SIMIYU
MAFUNZO kwa ajili ya walimu wa masomo ya sayansi mkoani Simiyu, yameingia dosari baada ya walimu kugoma wakidai posho.
Walimu 200 kutoka wilaya tano za mkoa huo, wanashiriki mafunzo hayo yenye lengo la kuwajengea uwezo, ambapo jana waligoma kuendelea wakitaka kufahamu mustakabali wa posho za kijikimu.
Habari za kuaminika zinasema walimu hao walifikia uamuzi huo baada ya kuhudhuria mafunzo hayo ya siku 10 kwa siku nne mfululizo bila kulipwa, hivyo kuwaweka kwenye mazingira magumu.
Jana, walimu 175 walisusa kuendelea na mafunzo hayo yanayofanyika katika Shule ya Sekondari ya Bariadi, wakitaka ufafanuzi kutoka kwa wakubwa walioandaa mafunzo.
Wakizungumza na waandishi wa habari, walimu hao walisema barua za mwaliko ziliwaeleza semina itakuwa ya siku 10, lakini walishangazwa kupunguzwa siku hizo hadi kufikia tano.
Walisema wamekuwa wakiishi maisha ya shida bila kulipwa posho za kujikimu tangu walipofika huku wahusika wakiwapiga change bila kuwaeleza kinachoendelea.
Mwalimu Masaga Sitta, alisema wanashangazwa na hatua ya uongozi wa mkoa kukataa kuwaona wala kusikiliza kilio chao kuhusiana na posho hizo.
“Tunashangazwa sana na uongozi wa idara ya elimu. Wamekuja  kututelekeza na kutuaibisha tu bila sababu. Ni semina gani isiyotoa mwongozo na maelekezo vizuri kwa washiriki. Wanatupa  shaka na hali hii inatufanya tufikirie fedha zetu zimechakachuliwa,” alisema.
Naye Mwalimu Mujo Meli alisema kitendo hicho si kizuri kwa kuwa kila wanapohoji kuhusu na posho hizo, hutolewa kauli za dharau na kejeli, jambo ambalo ameliita kuwa ni udhalilishaji.
“Tangu tumefika hapa tunadaiwa katika hoteli tunazoishi lakini tumeamua kutoendelea na mafunzo bila kukaidi ila hawatupi majibu ya msingi. Sasa hatushiriki tena mpaka kieleweke,” alisema Meli.
Akizungumza madai hayo, Ofisa Elimu Mkoa wa Simiyu, Alois Kamamba, alikiri kuwepo kwa mgomo huo akisema umetokana na kuchelewa kwa mhasibu kutoka makao makuu ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi.
“Ni kweli walimu waligoma na walikuwa na haki kweli ya kugoma maana tangu wamefika katika semina siku ya nne sasa, hatujawalipa kweli na walikuwa wanadaiwa. Tatizo ni mhasibu alichelewa kufika, kwa sasa ameishafika tutawalipa,” alisema Kamamba.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru