Sunday 26 October 2014

Sekta ya anga yakabiliwa na uhaba wa wafanyakazi


NA MWANDISHI WETU
MAMLAKA ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA),  imetoa wito kwa wanafunzi wote nchini kusoma masomo yatakayowawezesha kufanya kazi katika sekta ya anga.
Imeelezwa kuwa sekta hiyo hivi sasa inakabiliwa na uhaba mkubwa wa wataalam.
Rai hiyo ilitolewa jana na Mwanasheria Mkuu wa TAA, Wakili, Ramadhani Maleta alipokuwa akihutubia katika mahafali ya nne ya Shule ya Sekondari ya Lilian Kibo, Goba Matosa, Dar es Salaam.
Maleta alisema ni aibu kwa  mamlaka kuajiri wataalam kutoka nje ilhali wanafunzi wana uwezo wa kusoma na kufaulu vizuri.
 “Mamlaka ya Viwanja vya Ndege inategemea sana juhudi zenu ili tuweze kupata wataalam wakiwemo marubani, wahandisi, waongoza ndege, wanasheria na wahudumu wa kwenye ndege,” alisema.
 “Natoa rai kwa vijana mnaomaliza na hata ambao bado mpo katika vidato vya chini, mwongeze juhudi katika masomo yenu, kwani taifa na hata sisi tulio katika sekta ya usafiri wa anga tunawategemea muwe wataalam wetu hapo baadaye,” alisema na kuongeza kuwa sekta hiyo hivi sasa inakuwa kwa kasi nchini.
Aliupongeza uongozi wa shule hiyo kwa kazi nzuri ulioifanya ya kuwalea vijana kielimu na kufanikisha kupeleka vijana wote 22 wa kidato cha sita katika vyuo vikuu vya Mzumbe, Sokoine, SAUT, Dar es Salaam, Chuo cha Uhasibu (TIA), IFM baada ya kufaulu kwa daraja la kwanza na la pili tu katika masomo ya sayansi na sanaa mwaka 2013.
TAA imeahidi kuchangia sh. milioni tano kwa ajili ya kuvuta maji ya bomba shuleni hapo. Hata hivyo iliwataka wazazi kuchangia mfuko wa maji

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru