Monday 27 October 2014

Vyeti vilivyopotea kulipiwa sh. 100,000


NA RACHEL KYALA
BARAZA la Mitihani la Tanzania (NECTA), limeanzisha utaratibu wa kutoa nakala za vyeti kwa watahiniwa waliopoteza vyeti vyao kwa gharama ya sh. 100,000.
Utaratibu huo utawanufaisha watahiniwa waliohitimu kuanzia mwaka 2008, ambao vyeti vyao viliwekwa picha.
Katibu Mtendaji wa NECTA, Dk. Charles Msonde, akizungumza jijini Dar es Salaam jana, alisema hatua hiyo itapunguza changamoto zilizokuwa zikiwakabili watahiniwa waliopoteza vyeti vyao kwa sababu mbalimbali.
"Baraza limeweka utaratibu madhubuti ili kuhakikisha fursa hii haitumiwi vibaya, ikiwemo kufanya uchunguzi wa uhalali wa mwombaji, taarifa ya upotevu wa cheti katika kituo cha polisi na kutangaza gazetini, vielelezo husika vilivyoambatanishwa," alisema. 
Hata hivyo, alisema yeyote aliyepatiwa cheti mbadala, atatakiwa kurejesha cheti hicho iwapo cheti cha awali kitapatikana.
Aliongeza kuwa iwapo baraza litabaini udanganyifu wa aina yoyote katika maombi hayo, wahusika watachukuliwa hatua za kisheria.
Dk. Msonde aliwashauri waajiri kufuatilia NECTA uhalali wa vyeti vya watu wanaopita kwenye usaili kabla ya kuwaajiri ili kukomesha tatizo sugu la waajiriwa kughushi vyeti.
Alisema NECTA kwa kushirikiana na kamati za uendeshaji mitihani katika ngazi za mikoa, wilaya na wasamaria wema, wamefanikiwa kudhibiti wizi na udanganyifu wa mitihani ya taifa.
Alifafanua kuwa katika mtihani wa kumaliza elimu ya msingi (PSLE), mwaka 2013 takwimu, zinaonyesha kuwa watahiniwa waliofutiwa matokeo kwa kufanya udanganyifu ni 13 tu, ikilinganishwa na watahiniwa 9,736, mwaka 2011 na 293 mwaka 2012.

1 comments:

  1. Naweza kulipia cheti change kilichopotea kwa njia gani maana mi nipo mkoani

    ReplyDelete