Monday 27 October 2014

Prof. Mwandosya awapa somo viongozi wa dini


 Na Rhoda Ezekiel, Kigoma
MAASKOFU na viongozi wengine wa dini wametakiwa kusoma na kuelewa kipengele kinachohusu haki na uhuru wa kuabudu katika Katiba Inayopendekezwa.
Kufanya hivyo kutawawezesha kuwafahamisha waumini wao haki na uhuru huo kama inavyopendekezwa katika Katiba hiyo pasipo kuingiliwa na mtu yeyote.


Kauli hiyo ilitolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Profesa Mark Mwandosya, katika sherehe ya kumsimika askofu wa nne wa Jimbo la Kigoma,  Askofu Joseph  Mlolwa.
Alisema katika rasimu iliyo pendekezwa imeweka uhuru kwa kila mtu kuchagua dini yoyote pasipo kuingiliwa.
Profesa Mwandosya alisema katika rasimu inayopendekezwa ibara ya 19 kifungu cha 41 kinaelezea uhuru wa mtu kuabudu na kuamini imani anayotaka mradi asikiuke sheria za nchi.
“Nchi yetu haina udini tangu ilipoanzishwa mpaka ilipofikia sasa , na tutaendelea kumuenzi Baba wa Taifa (Mwalimu Julius Nyerere)  kwa kukemea udini na ukabila katika nchi yetu,” alisema  Mwandosya.
Aidha alisema serikali inatambua umuhimu na mchango wa makanisa na misikiti kwa kuendelea kuisaidia serikali katika nyanja za kijamii kama shule, hospitali pamoja na vituo vya kuhifadhi watoto wanaoishi katika mazingira magumu.
Hata hivyo aliwaomba viongozi wadini kuendeleza umoja na mshikamano  na kuepukana na uchochezi utakaosababisha kuvurugika kwa amani.
Kwa upande wake Askofu Mlola, alimshukuru kiongozi huyo na kuahidi kushirikiana na serikali kuhakikisha amani inaendelea kuwepo nchini.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru