Sunday 26 October 2014

Profesa Mwandosya alonga


NA SOLOMON MWANSELE, MBEYA
ALIYEKUWA mjumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, Profesa Mark Mwandosya, amesema suala la wabunge kuwajibishwa na wananchi, halipo katika katiba ya nchi yoyote duniani.
Imeelezwa wajumbe wa Bunge hilo waliangalia na kuzipitia katiba nyingi, lakini hawakuona hata moja  iliyowapa uwezo wananchi kumwajibisha mbunge.
Profesa Mwandosya aliyasema hayo, alipokuwa akijibu swali aliloulizwa kwanini katiba iliyopendekezwa haikuweka kifungu hicho kama wananchi walivyopendekeza katika tume ya Jaji Warioba.
Alisema maoni ya awali ya wananchi yalikuwa ni mwanzo wa utaratibu wa kupata katiba na si hatua ya mwisho. “ Ingekuwa hivyo kusingekuwa na haja ya kwenda kwenye kura ya maoni, hata Bunge kuketi,” alisema.
 “Tume ya Jaji Warioba  haikuwa kura ya maoni tafadhali sana, wale walioweza kutoa maoni walitoa, lakini wengi zaidi hawakutoa. Watu wengi zaidi watakuja kutoa maoni yao kwa kutoa uamuzi kusema ndiyo au hapana,” alisema Profesa Mwandosya.
Alisema anachojua, wananchi wanawawajibisha wabunge wakati wa uchaguzi, kama mbunge hakutekeleza ahadi, pale anaweza kuwajibishwa kwa kutochaguliwa tena.
Kwa mujibu wa Mwandosya, kila baada ya uchaguzi mkuu kufanyika, zaidi ya nusu ya wabunge wanaondoka, hivyo wananchi wanakuwa wamewawajibisha na kuwa huo ni mfumo tu na wabunge wabovu hawataendelea kubaki hata siku moja.

Alisema  mwaka 2010, zaidi ya asilimia 60 ya wabunge waliokuwepo mwaka 2005, waliwajibishwa na wananchi kwa kunyimwa kura.
Profesa Mwandosya alibainisha kuwa  hivi sasa idadi ya wabunge waliopo bungeni tangu mwaka 2000,  hawazidi 20 .

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru