Tuesday 18 February 2014

TAMWA kuzindua ripoti utafiti wa kijinsia

Na Mwandishi wetu

CHAMA cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA), leo wanatarajia kuzindua ripoti ya utafiti wa kijinsia uliofanyika Desemba, mwaka jana katika wilaya 20 za Tanzania.
Ripoti hiyo inatarajiwa kuzinduliwa katika ofisi za TAMWA zilizoko Sinza Mori, Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, Valerie Msoka, alisema jana kuwa uzinduzi huo unatokana na utafiti uliofanyika baada ya mafunzo kutolewa kwa waandishi wa habari  juu  ya habari za uchunguzi kuhusu a ukatili wa kijinsia, chini ya ufadhili wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Idadi ya watu UNFPA.
Alisema ripoti hiyo ya utafiti inaonyesha hali halisi ya unyanyasaji wa kijinsia katika jamii pamoja na mambo yanayokwamisha juhudi za vyombo vinavyotetea haki za wanawake na watoto hapa nchini.
Kwa mujibu wa Valerie, utafiti huo ulifanywa kwa kushirikiana na waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali.
Mkurugenzi Mtendaji huyo alisema waandishi wa habari waliweza kuwahoji wanajamii mbalimbali kuanzia ngazi za familia na kupata ukweli wa hali halisi ya unyanyasaji wa kijinsia ikiwemo, ukeketaji, ubakaji, mauaji ya vikongwe, mimba katika umri mdogo na watoto wa kike kulazimishwa kuolewa.
Wilaya ziliyofanyiwa utafiti ni Kahama (Shinyanga), Tarime (Mara), Sengerema (Mwanza), Newala (Mtwara), Mbulu (Manyara), Singida Vijijini (Singida), Bariadi (Simiyu), Busega (Simiyu), Nkasi (Rukwa), Dodoma (Dodoma), Babati (Manyara), Chunya (Mbeya) na Bunda (Mara).
Kwa upande wa Zanzibar utafiti ulifanywa katika wilaya sita za mikoa ya Mjini Magharibi, Kusini Pemba, Kaskazini Pemba, Unguja Kusini na Kaskazini Unguja.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru