Wednesday 18 December 2013

Abiria 213 wanusurika kifo


NA LILIAN JOEL, Arusha
NDEGE kubwa ya Shirika la Ethiopia Air Line, aina ya Boing 767 imetua kwa dharura katika uwanja mdogo wa Arusha.
Hatua hiyo inatokana na kushindwa kutua Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA), kutokana na ndege nyingine ya Shirika la TFC kupata pancha kwenye njia ya kuruka na kutua ndege katika uwanja huo.

Ndege hiyo Boing 767 yenye namba ET- AQW iliyokuwa ikitoka Ethiopia ilitakiwa kutua KIA, lakini kutokana na kuwapo iliyopata hitilafu, rubani alitakiwa kwenda kutua Uwanja wa Ndege wa Jomo Kenyatta, nchini Kenya.
Hata hivyo, imeelezwa kutokana na ndege hiyo kutokuwa na mafuta ya kutosha, rubani alilazimika kutua uwanja mdogo wa Arusha.
Ndege hiyo ilitua saa 6.52 mchana lakini kutokana na udogo wa uwanja huo, ililazimika kutua kwenye tope.
Wakati ndege hiyo ikitua, kulizuka taharuki miongoni mwa wafanyakazi wa uwanja huo na abiria waliokuwa wakisubiri kusafiri kwa ndege za kampuni nyingine.
Baada ya kutua salama, abiria zaidi ya 213 waliokuwa ndani ya ndege hiyo na wafanyakazi 23 walitakiwa kushuka kwa kutumia ngazi za Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) zilizofungwa kwenye gari la zimamoto lakini walikataa.
Kutokana na hilo, walilazimika kukaa ndani kwa zaidi ya saa tano wakisubiri ngazi kubwa kutoka KIA. Milango ya dharura ililazimika kufunguliwa ili abiria wapate hewa.
Abiria aliyeamua kushuka kwa kutumia mlango wa dharura akiwa nje aliwasha sigara lakini aliombwa na mhudumu wa ndege hiyo kuizima na kurudi ndani.
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magesa Mulongo, aliyefika eneo la tukio saa moja baada ya ndege kutua, alisema hilo ni changamoto kubwa kwa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), kuangilia jinsi ya kuboresha uwanja huo.
Alisema rubani aliuona uwanja huo alipokuwa akiendelea kuwasiliana na waongoza ndege wa Jomo Kenyatta.
UWANJA WAFUNGWA
Kutokana na ukubwa wa ndege hiyo,  sehemu ya nyuma ilikuwa kwenye njia ya kuruka na kutua ndege, hivyo uwanja ulifungwa kwa saa kadha, huku abiria waliokuwa uwanjani wakishindwa kuendelea na safari.
Raia wa Uingereza Joachim Leon, alisema kwa zaidi ya saa tano walikwama kwenda Serengeti kutokana na njia kuzibwa.
MASHUHUDA WALONGA
Baadhi ya watu walioshuhudia tukio hilo jijini Arusha na viunga vyake walisema haijawahi kutokea kwa ndege kubwa kama hiyo kuruka chini chini, huku kukiwa na mngurumo mkubwa uliozua taharuki.
“Nilikuwa dukani nikaona ndege kubwa ikipita chini sana tofauti na tulivyozoea kuona ndege nyingine. Pia ilikuwa inayumbayumba hali iliyotufanya tupige kelele kwa kuhofia kuangukiwa na ndege hiyo,” alisema mwanamke aliyejitambulisha kuwa Mama Best.
Umati ulijitokeza nje ya uzio wa uwanja kuiangalia ndege hiyo.
Mkazi wa Arusha, Annet Josia, alisema amekuwa nje ya uwanja huo kwa zaidi ya saa tano akisubiri kumpokea kaka yake ambaye ni abiria wa ndege hiyo.
Maofisa wa Idara ya Uhamiaji walifika uwanjani hapo saa tisa alasiri kwa ajili ya utaratibu wa kikazi.
ABIRIA WAKUBALI KUSHUKA
Baada ya kusubiri kwa takriban saa tatu bila ngazi waliyokuwa wanahitaji kuletwa kutoka KIA, abiria hao waliwalazimisha wahudumu wa ndege hiyo kuwaruhusu washuke,  ambapo walitumia mlango wa dharura.
Baadhi walishuka wakiserereke kupitia kwenye mabawa ya ndege hiyo na kupokewa na wahudumu wa uwanja wa Arusha.
Akizungumza baada ya kushuka katika ndege hiyo Glory Maeda, alisema anamshukuru Mungu kwa kushuka salama, licha ya taharuki kubwa baada ndege kushindwa kutua KIA na kutokuwa na mafuta ya kufika Jomo Kenyatta.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru