Saturday 21 December 2013

Nape apumua kuwajibishwa mawaziri


NA BASHIR NKOROMO
KATIBU wa NEC ya CCM (Itikadi na Uenezi), Nape Nnauye amesema amepokea kwa faraja hatua ya mawaziri wanne kuenguliwa nyadhifa zao kwa ridhaa ya Rais Jakaya Kikwete.
"Najisikia vizuri, maana kwa kitendo cha mawaziri hao wanne kuchuliwa hatua naamini kitasaidia wale wengine waliolala nao waamke. Bila shaka sasa hakuna atakayelala na akilala anajua itakula kwake," alisema Nape akijibu swali la mtangazaji wa Kituo cha luninga cha ITV, mjini Dar es Salaam, jana.
Awali, mtangazaji wa luninga hiyo, Emmanuel Buhohela alitaka kupata mawazo ya Nape akiwa kiongozi wa ngazi ya juu wa Chama kuhusu hatua ya Bunge kushinikiza na hatimaye Rais kuwawajibisha mawaziri hao kwa kuridhia kutengua uteuzi zao, juzi.
Mawaziri waliofutiwa uteuzi wao na Rais na nafasi walizotoka zikiwa kwenye mabano ni, Dk. Emmanuel Nchimbi (Waziri wa Mambo ya Ndani), Shamsi Vuai (Waziri wa Ulinzi), Mathayo David Mathayo ( Mifugo na Maendeleo ya Uvuvi) na Khams Kagasheki (Maliasili na Utalii) ambaye ndiye pekee pamoja na uteuzi wake kutenguliwa na Rais, lakini alitangaza kujiuzulu akiwa bungeni.
Nape alisema pamoja na mawaziri hao kuwajibika, ipo haja ya kwenda mbali zaidi kwa kutazama mifumo na sheria zilizopo sasa kwa kuwa inaonekana ni miongoni mwa vyanzo vya vikwazo katika utekelezaji wa utawala bora.
"Kwa mfano leo hii, mawaziri wameng'oka, sawa ni jambo jema. Sitetei, lakini inawezekana kabisa kuna mifumo na sheria ambazo zilimkwaza waziri huyu kutimiza wajibu wake. Mfano, alihitaji kumfukuza mtu kazi kwa kuzembea jambo fulani, lakini mamlaka ya kufukuza kazi mtumishi yapo kwa Katibu Mkuu wa Wizara, hapa atafanyaje?" alihoji Nape na kuongeza;
"La msingi hapa ni lazima sasa hatua hizi ziende mpaka chini huko kwa watendaji ili isiwe mawaziri wanawajibishwa tu kwa sababu ya dhamana zao za kusimamia kisiasa, huku watendaji wanazidi kuvuta shuka bila hofu wakati baadhi yao ni sehemu ya matatizo".
Akijibu swali kuhusu ziara za Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana na Sekretarieti ya Chama mikoani, alisema ndiyo kwanza zimeanza na moto zaidi unakuja hasa utakapokaribia uchaguzi mkuu wa 2015.

Nape alisema ziara hizo zimeonyesha matunda makubwa kwa kuwa zimesaidia kupunguza kero nyingi katika maeneo zilikofanyika.
Alitoa mfano wa ziara hiyo ilivyoweza kuondoa msongamano wa malori wilayani Tunduma mkoani Mbeya, akisema wakati Kinana na msafara wake unaingia sehemu hiyo ulikuta msongamano mkubwa kutokana na wafanyakazi wanaohudumia malori  kufanya kazi kwa muda mfupi.
"Baada ya kuiagiza serikali isimamie wafanyakazi wa eneo hilo wafanye kazi kwa saa 24, kwa zamu, siku ya pili yake ya agizo hilo msongamano ulionekana kupungua sana na kuleta nafuu kwa madereva na wafanyabiashara kwa ujumla," alisema Nape.
Akizungumzia wabunge wanaodaiwa kulipwa posho bila kuzifanyia kazi, Nape alisema kurudisha fedha pekee hakutatosha, kwa upande wa CCM ambayo ndiyo yenye wabunge wengi itabidi ichukue hatua zaidi dhidi ya waliohusika bila kumuonea mtu.
Alisema katika uchaguzi ujao CCM itakomba viti vyote vya ubunge na udiwani vililivyoko chini ya vyama vya wapinzani, baada ya wapinzani kujaribiwa na kushindwa kuonyesha matunda yoyote ya kusaidia wananchi na hivyo kutokuwa mbadala wa CCM.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru