Saturday 21 December 2013

Walipa kodi 200,000 kutumia EFD


NA MWANDISHI WETU, DODOMA
SERIKALI imelenga kuingiza walipa kodi 200,000 kati ya 1,500,000 waliopo ili waweze kutumia mashine za kieletroniki za kutoa risiti (EFD).
Wafanyabiashara wadogo na wanaoendesha bishara zisizo rasmi kama vile wamachinga na wanaotembeza bidhaa barabarani na mama lishe hawatahusika na utaratibu huo.
Kauli hiyo ilitolewa bungeni jana na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, alipokuwa akiahirisha mkutano wa Bunge, mjini hapa.
Pinda alisema walengwa wa utaratibu huo ni wafanyabishara wakubwa wenye biashara zenye mtaji wa kati ya sh. milioni 14 na sh milioni 40.
Alisema ingawa kumekuwa na malalamiko juu ya bei kubwa ya mashine hizo, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) inaendelea kujadiliana na wasambazaji wa mashine hizo ili kuona uwezekano wa kushusha bei.
Waziri Mkuu alisema kwa kutumia mashine hizo mfanyabishara anaweza kutuma taarifa zake za mauzo moja kwa moja kwenda ofisi ya TRA na mamlaka nyingine zenye mahitaji ya taarifa hizo.
Alisema mamlaka nyingine ni pamoja na EWURA, SUMATRA na Taasisi ya Taifa ya Takwimu na Benki Kuu (BoT).
Pinda alisema mashine hizo zinatumia lugha za Kiswahili na Kiingereza ambazo zinatumiwa na Watanzania wengi.
Alisema ili kuhakikisha ubora wa mashine hizo, watengezaji wametoa muda wa miaka mitatu wa kutengeneza bure mashine itakayoharibika katika kipindi hicho bila kukusudia.
Kwa mujibu wa mkataba ulioingiwa kati ya wasambazaji na TRA, wasambazaji wanawajibika kuzifanyia matengenezo mashine hizo kila zinapoharibika ili kuondoa usumbufu kwa watumiaji kutafuta watengezaji wao wenyewe.
“Kwa kutambua umuhimu wa mashine hizo katika kuongeza mapato ya ndani, serikali inaendelea kushughulikia malalamiko ya baadhi ya wafanyabiashara juu ya matumizi ya mashine hizo, “ alisema.
Bunge limeahirishwa hadi Mei 6, mwakani litakapokutana kwa ajili ya mkutano wa bajeti. Hata hivyo wabunge ambao ni wabunge wa Bunge Maalumu la Katiba watakutana litakapoitishwa bunge hilo.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru