Tuesday 24 December 2013

Kova: Watoto, walevi marufuku kuogelea


NA JUMANNE GUDE
POLISI Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, imepiga marufuku watoto na walevi kwenda kuogelea katika ufukwe wa Bahari ya Hindi wakati wa sikukuu za Krismasi na Mwaka Mpya.
Kamishna wa Polisi wa kanda hiyo, Suleiman Kova, alitoa onyo hilo jana alipozungumza kuhusu kuimarishwa ulinzi wakati wa sikukuu ya Krismasi leo.

Alisema ulinzi umeimarishwa maeneo yote ya jiji na kwenye ufukwe wa bahari kutakuwa na vituo vya polisi vya muda.
“Watoto wenye umri chini ya miaka 15 hawataruhusiwa kuogelea. Pia kuna baadhi ya watu wakishalewa wanataka kuogelea, hawa nao watadhibitiwa na askari,” alisema.
Aliwataka wananchi watakaokwenda ufukweni kuwa waangalifu au wawe na utaalamu wa kuogelea ili kuepusha vifo vinavyotokana na watu kushindwa kuogelea.
Kwa mujibu wa Kova, wamejiandaa vyema na watashirikiana na askari wa Zimamoto na Uokoaji, Wanamaji na Kikosi cha Usalama Barabarani kuhakikisha wananchi wanasherehekea sikukuu kwa amani.
Alisema wakati wa sikukuu nyumba zote za ibada, hususan makanisa yatalindwa kwa kushirikiana na kamati za ulinzi za makanisa.
Kova aliwataka wananchi watoe taarifa mapema kwa askari endapo watabaini kuna uvunjifu wa amani katika maeneo yao, ili hatua za kisheria zichukuliwe haraka.
Alitoa rai kwa madereva kuzingatia na kuzifuata sheria za usalama barabarani ili kuepuka ajali zinazoweza kutokea.
“Kuna baadhi ya madereva wamekuwa wakiendesha magari wakiwa walevi au kwa mwendo kasi, kikosi cha usalama barabarani kitawashughulikia,” alisema.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru