Saturday 28 December 2013

January awawezesha wapanda pikipiki Mza


NA MWANDISHI WETU, MWANZA
NAIBU Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba, amewamwagia neema vijana wa bodaboda mkoani  Mwanza kwa kuwapatia mikopo ya pikipiki 1,745.
Pia amewakatia bima ya maisha waendesha bodaboda 100 ili kuhakikisha wanafanya kazi yao katika mazingira salama
wanaposafirisha abiria katika maeneo mbalimbali.
Akizungumza katika semina ya masuala ya bima kwa wanachama wa Umoja wa Waendesha Pikipiki mkoa wa Mwanza, January alisema lengo ni kuwawezesha vijana wa kujiajiri na kuwa waajiri.
Semina hiyo iliyofanyika katika Uwanja wa Nyamagana ambapo vijana wa bodaboda zaidi ya 1,000 walikusanyika wakiwa wamevaa fulani zenye ujumbe usemao ‘boda boda ni ajira, lakini usalama kwanza’.
Alisema mchakato wa kuwawezesha waendesha pikipiki wa Mwanza ulianza miaka mitatu iliyopita baada ya kuombwa na
Mwenyekiti wa umoja wao, Makoye Kayanda.
January alisema lengo ni kuhakikisha vijana hao wanakuwa na ajira ya uhakika na usalama wa maisha yao kwani kwa sasa  pikipiki zao zina bima lakini wenyewe hawana bima.
Alichezesha bahati nasibu kwa kwa kuwasshindanisha waendesha pikipiki waliojiandikisha majina na namba za bodaboda zao, ambapo washindi 100 , walikatiwa bima ya sh. 5,000 kila mmoja kwa ajili ya kujilinda na safari.
January ambaye ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM, alisema ajali za pikipiki zinaua ambapo mwaka 2011 watu 695 walikufa kwa ajali hizo na mwaka jana idadi ya vifo ilifikia 930.
Alisema kupitia bima hiyo vijana watakaoumia watalipwa fedha za matibabu na akipata ulemavu wa kudumu atalipwa sh. milioni 10.
Kwa upande wake Mkuu wa mkoa wa Mwanza, Evarist Ndikilo, alimpongeza January kwa jitihada za kuwawezesha vijana hao na kuwataka kufanya kazi kwa kujiwekea malengo ya kufanya kazi zingine, kwa kuwa pikipiki ni kazi ambayo
inafanywa na vijana na sio wazee.
Mapema Mwenyekiti wa vijana hao, Kayanda, alisema January ametimiza ndoto za vijana hao kwa kuwa wengi wao wameajiriwa na watu na wamekuwa wakifukuzwa kazi bila taarifa na kusababisha maisha yao kuyumba.
Katika semina hiyo iliyoshirikisha kampuni za bima za NIC na Ndege, January alikubali ombi la kuwa mlezi wa umoja wa waendesha bodaboda ambao una wanachama zaidi ya 400 mkoani huo.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru