Saturday 21 December 2013

Watu 10 washikiliwa mauaji ya Mabina


NA PETER KATULANDA, MWANZA
WATUHUMIWA wanaoshikiliwa kwa tuhuma za mauaji ya aliyekuwa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mwanza na Diwani wa Kata ya Kisesa wilayani Magu, Clement Mabina, wameongezeka na kufika 10.
Kamanda wa Polisi mkoani Mwanza, Valentine Mulowola, alisema jana kwamba, watuhumiwa wengine watatu tofauti na saba waliokamatwa awali walikamatwa kwa nyakati tofauti kufuatia upelelezi unaoendelea kufanywa na makachero.
“Hadi sasa tunawashikilia watu 10 kuhusiana na mauaji hayo ya kujichukulia sheria mkononi na ya kikatili. Bado tunaendelea na uchunguzi wa kina, tutawapeni taarifa. Nawaomba wananchi waendelee kuwa watulivu na kuendelea na shughuli zao za uzalishaji,” alisema.
Bila kuwataja watuhumiwa hao, alisema watu hao watatu walikamatwa katika maeneo mbalimbali tofauti ambayo hakuyataja.
Mabina aliuawa kikatili na kundi la baadhi ya wakazi wa Kisesa na Kanyama, Desemba 15, mwaka huu, mchana, kufuatia mgogoro wa kugombea eneo la mlima wa Kanyama ambalo alikuwa akilimiliki kwa hati.
Katika hatua nyingine, Mbunge wa Magu, Dk. Festus Limbu, aliagua kilio msibani huku akisisitiza kuwa hatagombea tena nafasi hiyo katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.
Dk. Limbu alilia juzi wakati akitoa salamu za rambirambi kwenye ibada ya misa ya mazishi ya Mabina, iliyofanyika kwenye Uwanja wa Chama Cha Msalaba Mwekundu Kisesa na kuongozwa na Paroko wa Parokia ya Bujora, Padre Fabian Mhoja.
“Kuna maneno maneno yanazunguka kwamba Limbu sasa amesema hagombei ubunge, nasema mwaka 2015 sigombei naomba mnielewe hivyo na msiniulize maswali kwa nini,”alisema mbunge huyo.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru