Wednesday 18 December 2013

Sakata la posho Kombora la Mwigulu lamchakaza Mbowe


“Rejea mazungumzo bwana Kabunju kuhusu Joyce Mukya, ambaye yupo safarini nitashukuru kama utambadilishia booking aweze kurudi, aondoke New York Desemba Mosi na aje Dubai, by Mbowe Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni
Na Theodos Mgomba, Dodoma
MBUNGE wa Iramba Mashariki, Mwigulu Nchemba (CCM), amemlipua Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe, kwa kuhusika kwenye matumizi mabaya ya fedha za umma.
Mwigulu alieleza bungeni jana kuwa, Mbowe (CHADEMA) alimrudisha mbunge wake, Joyce Mukya, aliyekuwa kwenye ziara ya kikazi na kumtaka kukutana naye Dubai.
Kombora hilo la Mwigulu limetolewa wakati wabunge wakituhumiwa kuchukua posho za safari bila kwenda kwenye maeneo wanayotakiwa, badala yake kuzitumia kwa matanuzi binafsi.
Bunge limewataka wabunge wote waliochukua posho za safari bila kusafiri kurejesha mara moja fedha hizo, ambazo ni mali ya walalahoi.
Hali ilianza kuwa tete baada ya Mwigulu kusimama na kuomba Mwongozo wa Mwenyekiti kuhusu baadhi ya wabunge, wakiwemo viongozi wa vyama vya siasa kutuhumiwa kuchukua posho na kutokwenda safari.
Mwigulu alisema Mbowe alimrejesha Joyce kutoka nchini Marekani na kwenda kwa muda Dubai.
“Mheshimiwa Mwenyekiti baadhi ya magazeti leo (jana) yameandika kuwepo baadhi ya wabunge waliolipwa fedha za safari, lakini hawakwenda. Jambo hili linachafua taswira ya Bunge zima.
“Wengine tuna maadili ya uongozi, magazeti mengine yameandika kuna kigogo mmoja amemzuia hawara yake kusafiri na alikuwa amelipwa kila kitu na hakusafiri, hili ni jambo binafsi.
“Na nina ujumbe nimeupata Kiongozi wa Kambi ya Upinzani humu bungeni akimwandikia mtumishi wa Bunge kuwa:
‘Rejea mazungumzo bwana Kabunju kuhusu Joyce Mukya ambaye yupo safarini nitashukuru kama utambadilishia booking yake aweze kurudi, aondoke New York Desemba Mosi na aje Dubai, lakini baadaye ataunganisha na kurejea  Dar es Salaam by Mbowe Kiongozi wa kambi ya Upinzani bungeni nakala kwa Joyce Mushi’.
“Haya ni mambo binafsi, naomba kujua ofisi yako inasema nini kwa mbunge aliyetumwa kuwakilisha taifa halafu mtu binafsi kwa kutumia nafasi yake anamrudisha, mtu ambaye ametumia fedha za serikali anamuita Dubai kwa kazi yake binafsi, taifa langu lina bahati mbaya kiasi gani,” alisema.
Aliongeza: “Naomba mwongozo wako juu ya hatua stahili ya kupambanua wabunge wa namna hii na hatua stahili kwa mbunge kuingilia kazi za kiti na hatua stahili kwa watumishi wa bunge wanapoingiliwa.’’
Kauli ya Mwigulu iliamsha miongozo kutoka kwa Mwenyekiti wa Bunge, ambapo David Silinde (Mbozi Magharibi -CHADEMA), alisimama na kueleza kuwa, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mbeya, Godfrey Zambi, aliwahi kuchukua fedha, lakini hakwenda safari na Kamati yake ya Hesabu za Serikali (PAC).
“Mheshimiwa Mwenyekiti naomba mwongozo wako, suala la kuchukua fedha na kutokwenda safari lisiangaliwe kwa upande wa upinzani tu, hata Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mbeya naye aliwahi kuchukua fedha na hakwenda safari na kamati yake.
“Cha kufanya Mwenyekiti ni kwa namna gani Bunge lako litachukua hatua na iwapo wabunge wengi tu ambao ni wajumbe hapa wanawajua wanaochukua fedha, lakini hawaendi,” alisema.
Katika harakati za wabunge wa CHADEMA kumuokoa Mbowe, Mariam Msabaha (Viti Maalumu), alisimama kuomba mwongozo na kusema kuna baadhi ya watu wameandikwa katika magazeti kuwa wameiba vidani.
“Mheshimiwa Mwenyekiti mimi ni mtu mwenye nidhamu na huwa sisimami mara kwa mara, lakini leo naomba niseme kuna watu humu wameandikwa kuwa wameiba vidani mbona hawasemwi, mambo ya mapenzi kila mtu na mpenzi wake, kuna mambo mengi yanafanyika humu bungeni mbona hayasemwi,’’ alisema.
Zitto Kabwe (Kigoma Kaskazini -CHADEMA), alisimama kuomba mwongozo akisema ni jambo la aibu kwa Bunge kuingia katika matumizi mabaya ya fedha za serikali.
Alisema tayari Kamati ya Hesabu za Serikali imeshamuomba Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kukagua safari zote za wabunge na kutoa taarifa kwa Spika, na kama itaonekana inafaa taarifa hiyo iwasilishwe bungeni kujadiliwa.
“Mheshimiwa Mwenyekiti ni jambo la aibu kwa Bunge kuingia katika mgogoro namna hii wa matumizi mabaya ya fedha na hii inaonyesha taswira mbaya kwa wananchi.
“Tayari kamati imemuomba CAG kufanya uchunguzi wa safari zote na kutoa taarifa. Kamati itapeleka kwa Spika na kama ataona inafaa italetwa bungeni ili mambo hayo tuweze kuyamaliza, ni aibu,’’ alisema.
Akijibu miongozo hiyo, Mwenyekiti wa Bunge, Mussa Zungu, alisema wabunge wote waliochukua fedha za safari na hawakwenda ni lazima wazirejeshe.
Zungu alisema tayari malalamiko hayo yamefikishwa mezani kwa Spika wa Bunge, Anne Makinda na yanaendelea kushughulikiwa.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru