Wednesday 18 December 2013

Walinzi wa mgodi wadaiwa kuua raia


NA MARCO KANANI, GEITA
WALINZI wa mgodi wa dhahabu wa GGM mkoani Geita, wanadaiwa kumpiga hadi kufa Emmanuel Mwita, ambaye aliingia kwenye eneo la mgodi kuokota mawe ya dhahabu.
Habari za kuamini zilisema Mwita (32), aliingia kwenye eneo hilo kuokota mawe yaliyokuwa yamemwagwa katika vifusi.
Tukio hilo linadaiwa kutokea juzi saa 7:00 usiku, ambapo walinzi hao walimkamata na kuanza kumshambulia hadi kumsababishia kifo.
Akizungumza kwa sharti la kutotajwa jina gazetini, mmoja wa vijana waliokwenda kuokota mawe na Mwita, alisema wakiwa eneo la tukio, walikurupushwa na walinzi.
Alisema baadhi walifanikiwa kutoroka, lakini Mwita alikamatwa na kuanza kupigwa sehemu mbalimbali za mwili.
“Tulisikia mwenzetu akilia na kuomba msaada na kuwataka walinzi hao wasiendelee kumshambulia, lakini hawakufanya hivyo na badala yake walizidi kumshambulia,’’ alisema.
Alisema siku iliyoafuata walienda Kituo cha Polisi Geita ili kufahamu kama mwenzao alifikishwa kituoni hapo, lakini walielezwa kuwa hakufikishwa.
“Tulikwenda hospitali zote ili kupata taarifa, lakini hakuwepo ndipo baadaye tukaelezwa kuwa kuna mgonjwa ameletwa na kutelekezwa na askari wa GGM ana hali mbaya. Baadaye tukaelezwa kuwa amefariki dunia,’’ alisema.
Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hospitali Wilaya ya Geita, Adamu Sijaona, alisema mwili wa Mwita ulikuwa na jeraha kubwa kichwani na alikuwa ametokwa na damu nyingi.
Pia, alisema baadhi ya viungo vyake ikiwemo mikono ilikuwwa imevunjika.
Hili ni tukio la pili kutokea ndani ya miezi miwili, ambapo Oktoba 17, mwaka huu, walinzi hao wa mgodi walidaiwa kumuua Zakaria Thobias (35) kisha kumwekea jiwe kubwa kifuani kwa lengo la kuficha ushahidi.
Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani Geita Amina Baturumili, alisema hajapata taarifa za tukio hilo na kuahidi kulifuatilia kwa karibu.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru