Saturday 28 December 2013

Wahimizwa kupeleka majina wajumbe bunge la katiba


Na Hamis Shimye
SERIKALI imewataka wananchi wanaoongoza makundi mbalimbali katika jamii kupeleka majina ya watu ambao wanaona yanafaa kuteuliwa na Rais Jakaya Kikwete kuwa wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba kabla haujafika.
Uamuzi huo, unatokana na taarifa ya Rais Jakaya Kikwete iliyotolewa na Ofisi ya Katibu Mkuu Kiongozi ikitoa mwaliko kulingana na mamlaka aliopewa Rais katika kifungu cha 22(1) (c) cha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba (Sura ya 83) ambapo mwaliko huo ulitangazwa katika Gazeti la Serikali Na. 443 la Desemba 13, mwaka huu.
Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe, alisema umeshatolewa muongozo wa namna ya kupatikana kwa wajumbe hao ambao watawakilisha wananchi, ambapo mwisho wa kupokea majina hayo ni Januari 2, mwakani.
Alisema bunge hilo linatarajiwa kuwa na wajumbe zaidi ya 200 kutoka makundi mbalimbali, hivyo wananchi wanapaswa kutuma majina yao kabla muda haujafika.
“Majina ya makundi yanayotakiwa kutumwa ni yale yaliyosajiliwa kisheria, ambapo watume majina yao. Kutakuwepo na wajumbe 20 kutoka katika taasisi mbalimbali zisizokuwa za kiserikali kati yao nusu wanatakiwa watoke Zanzibar wakiwemo wanawake na wanaume pamoja na wajumbe wengine 20 katika taasisi za kidini, wajumbe 40 kutoka vyama vya siasa vilivyoandikishwa na kusajiliwa,”alisema.
Hivi karibuni, Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue, alitoa taarifa ya mwaliko huo ambao pia ulitangazwa katika magazeti ya kawaida.
Makundi ambayo yametajwa katika Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ni taasisi zisizokuwa za kiserikali, taasisi za dini, yyama vyote vya siasa vyenye usajili wa kudumu, taasisi za elimu ya juu, makundi ya watu wenye ulemavu, vyama vya wafanyakazi, vyama vinavyowakilisha wafugaji, vyama vinavyowakilisha wavuvi, vyama vya wakulima na makundi mengine yenye malengo yanayofanana.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru