Saturday 28 December 2013

TAZARA wakamata meno ya tembo


NA MWANDISHI WETU
KIKOSI cha Polisi wa Mamlaka ya Reli Tanzania na Zambia (TAZARA) kinamshikilia Ally Juma baada ya kumkuta akisafirisha vipande 14 vya meno ya tembo na jino moja la kiboko.
Kaimu Kamanda wa Kikosi hicho, Innocent Mgaya, alisema mjini Dar es Salaam, jana, kuwa vipande hivyo vilikamatwa saa 12.15, jioni, Desemba 26, katika Stesheni ya Kisaki, Wilaya ya Morogoro.
Alisema vipande hivyo vilikuwa ndani ya treni ya abiria yenye namba M2 iliyokuwa ikitokea Zambia kwenda Dar es Salaam.
Mgaya alisema kwa mujibu wa maofisa wa wanyamapori kutoka Wizara ya Maliasi na Utalii, vipande hivyo vina thamani ya sh. milioni 25.5 wakati jino la kiboko ni sawa sh. milioni 2.4.
Alisema tukio hilo lilitokea wakati askari wao wa intelijensia wakiwa kazini katika eneo hilo walipopata taarifa kutoka kwa msamaria mwema kuwepo kwa mtu mwenye meno hayo.
Alisema vipande vya meno ya tembo vina uzito wa kilo 29, huku jino la moja kiboko lina uzito wa gram 900, ambapo vyote vilikutwa kwenye mabegi mawili na begi moja lilikuwa na vipande vinane huku lingine likiwa navyo saba.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru