Wednesday 18 December 2013

MUHAS inafadhiliwa na serikali -Waziri


CHUO Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) ni miongoni mwa vyuo vikuu vitano vya umma vinavyofadhiliwa na serikali.
Naibu Waziri wa Fedha, Saada Mkuya Salum, alisema hayo jana alipojibu swali la Deogratius Ntukamazina (Ngara -CCM), aliyetaka kujua ni lini serikali itakipa chuo hicho kipaumbele.
Saada alisema serikali imekuwa ikikifadhili chuo hicho kwa kugharamia wataalamu wake.
Alisema mwaka 2013/2014  wataalamu 295 walipata mafunzo, kati yao 195 waliendelezwa kwa kiwango cha Shahada za Uzamili.
Kwa mujibu wa Saada, wengine 100 waliendelezwa katika ngazi za Shahada ya Uzamivu.
Naibu waziri alisema MUHAS pia ni miongoni mwa vyuo vikuu sita vilivyofaidika na ufadhili wa Tume ya Sayansi na Teknolojia katika kugharamia mafunzo ya wataalamu 184.
Wataalamu hao walipata mafunzo katika ngazi za Shahada ya Uzamili na 84 katika ngazi za Shahada ya Uzamivu.
Alisema serikali pia imekuwa ikitoa udhamini kwa wanafunzi wa kozi za udaktari walioko katika vyuo binafsi.
Licha ya juhudi hizo, alisema serikali ilikwisharidhia mpango wa ujenzi wa Kampasi ya Mlonganzila, Dar es Salaam kwa ajili ya MUHAS.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru