Saturday 21 December 2013

Bunge la Katiba laiva .


Na Mwandishi Wetu
RAIS Jakaya Kikwete ameyaalika na kuyakaribisha makundi mbalimbali katika jamii kupendekeza majina ya watu ambao wanaona yanafaa kuteuliwa na Rais kuwa wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba.

Rais Kikwete ametoa mwaliko huo kulingana na mamlaka anayopewa katika kifungu cha 22(1) (c) cha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba (Sura ya 83) na aliutangaza rasmi mwaliko huo katika Gazeti la Serikali Na. 443 la Desemba 13, mwaka huu.
Taarifa iliyotolewa juzi mjini Dar es Salaam na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue, mwaliko huo ambao pia utatangazwa katika magazeti ya kawaida, makundi yaliyokaribishwa kutoa mapendekezo yametakiwa kuwasilisha kwa Rais orodha ya watu wasiopungua wanne na wasiozidi tisa kwa kila kundi.
Makundi hayo ambayo yametajwa katika sheria ya mabadiliko ya katiba ni taasisi zisizokuwa za kiserikali, taasisi za dini, vyama vyote vya siasa vyenye usajili wa kudumu, taasisi za elimu ya juu, watu wenye ulemavu, vyama vya wafanyakazi, vyama vinavyowakilisha wafugaji, vyama vinavyowakilisha wavuvi, vyama vya wakulima na makundi mengine yenye malengo yanayofanana.
Taarifa ya Balozi Sefue ilisema katika kuwasilisha mapendekezo ya majina yao, makundi yaliyoalikwa yanalazimika kuonyesha umri, jinsia, uzoefu, sifa na sehemu ya makazi ya mtu anayependekezwa ikiwa ni pamoja na kuzingatia usawa wa kijinsia.
Katika mwaliko wake, Rais Kikwete ameelekeza kuwa orodha ya majina ya wanaopendekezwa iwasilishwe kwa maandishi ama kwa kupelekwa na mtu kwa mkono ama kwa kutumia huduma ya Posta.
Ilisema orodha hizo ziwasilishwe kupitia anuani zifuatazo Katibu Mkuu Kiongozi Ofisi ya Rais, Ikulu, Katibu Mkuu Kiongozi, Ofisi ya Rais, ambapo mwisho wa kupokea orodha ya majina yanayopendekezwa ni Januari 2, mwakani.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru