Friday 19 July 2013

Ahukumiwa bakora 70 kwa kusema uongo


NA LILIAN JOEL, ARUSHA
KIJANA wa jamii ya Kimasai, Lomayani Mitewasi, amenusurika adhabu ya viboko 70 akituhumiwa kusambaza taarifa ya uongo kwenye mitandao ya kijamii.
Mitewasi alipewe adhabu hiyo juzi na viongozi wa jamii hiyo, pia aliamriwa kulipa ng’ombe dume kwa kosa la kukiuka mila za Kimasai.
Kijana huyo mkazi wa kata ya Elerai, alilazimika kusimama mbele ya wazee wa kimila (Malaigwanani) na kukiri kuwa taarifa hizo ni za uongo, na amekiuka mila za jamii hiyo kwa kuandika taarifa za uongo katika mitandao ya kijamii.
“Wazee wangu naomba mnisamehe nilighafilika ninakiri  kuandika habari za uongo katika mitandao hiyo. Sikijui Kimasai, huwa ninasikia neno mojamoja tu, ingawa nilikuwepo kwenye mkutano uliopita sikujua hata mlizungumza nini, kwa kuwa mlikuwa mnazungumza kilugha,” alisema.
Kwa mujibu wa kijana huyo, aliandika Malaigwanani wamegawanyika katika makundi mawili, moja linatetea CCM na lingine CHADEMA jambo ambalo ni uongo.
Pia aliandika Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Goodluck Ole Medeye, amewatumia Malaigwanani kuvuruga uchaguzi mdogo wa madiwani jijini Arusha.
Mitewasi aliandika kikao hicho kililenga kubagua wakazi wa Arusha kwa tofauti za makabila, ambapo alilazimika kufuta kauli na kuomba radhi mbele ya Malaigwanani hao kwa kile alichodai alighafilika.
Awali, akitoa taarifa kwa waandishi wa habari jana, Katibu wa Baraza la MAA, Amani Lukumay, alisema wazee hao wamesikitishwa na taarifa hizo za uongo, ambazo zilisambazwa katika mitandao ya kijamii.
Lukumay alisema lengo la taarifa hiyo ni kuvuruga amani ya Jiji la Arusha na kuwagawa wazee hao. Alisema kikao cha wiki iliyopita kililenga kuzungumzia amani na hakuna kingine kilichozungumzwa.
Katibu huyo alitoa ufafanuzi baada ya kikao chao cha wiki iliyopita kuelezwa kuwa kilikuwa kina mwelekeo wa kisiasa, uliolenga kuinufaisha CCM dhidi ya CHADEMA.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru