Monday 8 July 2013

Moto wazuka Mlima Kilimanjaro


NA MWANDISHI WETU
HEKARI 40 za Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro wilayani Rombo, zimeteketea moto, uliotokana na uvunaji haramu wa asali.

Taarifa iliyotolewa na Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), imesema moto huo ulizuka juzi, saa nane mchana, baada ya watu wasiojulikana kufanya uvunaji haramu wa asali kwa kutumia moto.
Kwa mujibu wa TANAPA, taarifa za awali zinaonyesha chanzo cha moto huo ni uvunaji haramu wa asali katika eneo la Amboni.
Imeelezwa watu hao waliingia hifadhini eneo la Amboni na kuvuna asali kwa kutumia moto, ambapo baada ya kusambaa walikimbia.
TANAPA imesema kwa kuwashirikisha wananchi wa maeneo jirani ya Mshiri, Lyasongoro, Amboni, Ushiri na Ikuwini, wanapambana kuuzima moto huo.
Taarifa hiyo ilisema askari wanafunzi kutoka Kikosi cha Kuzuia Ghasia (FFU) wapo njiani kwenda eneo la tukio kuungana na kikosi kilichopo eneo hilo ili kuzima moto huo.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru