Monday 29 July 2013

Ufadhili, rushwa unaharibu uchaguzi Afrika Mashariki


Na Anne Kiruku, EANA
KUKOSEKANA kwa utashi wa kisiasa katika vita dhidi ya rushwa katika Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), kunatokana na jinsi kampeni za uchaguzi wa kisiasa zinavyofadhiliwa.
Mkutano wa kanda uliofanyika mjini Kigali, Rwanda hivi karibuni, ulifafanua kuwa ufadhili huo umechochea upendeleo katika uteuzi wa nafasi mbalimbali za umma, utoaji wa tenda na mikataba mingine ya huduma za jamii.
Washirika wa mkutano huo, waliwataka viongozi wa EAC waongeze vita dhidi ya rushwa kwa kusimamia utawala bora na kuzingatia uwajibikaji, uwazi na utawala wa sheria na siyo maneno bila vitendo.
Mkutano huo pia ulipendekeza kuoanisha sheria zinazohusu vita dhidi ya rushwa katika kanda hiyo na kujumuisha kipengele cha uwajibikaji wa kisiasa.
Wakizungumzia athari hasi za rushwa, wajumbe hao waliambiwa kuwa ni kubwa zaidi kwa makundi yaliyo katika hali ya unyonge wakiwemo wanawake, watoto na masikini katika jamii.
“Ili kufikia lengo la kuwa na Afrika Mashariki yenye mafanikio na umoja wa kisiasa, wadau wote hawanabudi kuzingatia utaratibu wa uwazi na uwajibikaji,” walisema wajumbe wa mkutano huo.
Mkutano wa Nne wa Mwaka wa EAC juu ya utawala bora, umewaleta pamoja wajumbe kutoka serikali za nchi wanachama na wadau binafsi wanaojihusisha na masuala ya kukuza utawala bora.
Mkutano huo ulioandaliwa na EAC, uliunda jukwaa la majadiliano ya mambo muhimu yanayohusu utawala bora yanayogusa mwenendo mzima wa mtangamano wa Jumuiya.
Akifungua mutano huo, Spika wa Bunge la Rwanda, Rose Mukantabana, alikiri kuwa rushwa ni ‘kansa kwa maendeleo ya kiuchumi.’
Alisema inakandamiza demokrasia na kubeza utawala wa sheria, hivyo, aliwataka viongozi wa EAC, kutafuta njia mbadala ya kupambana nayo.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru