Tuesday 16 July 2013

Mapya yaibuka tozo ya simu


NA RABIA BAKARI
MALIPO ya tozo ya sh. 1,000 kwa kila kadi ya simu, yameibua mapya, ambapo maelfu ya wananchi wamepinga kulipa fedha hizo.
Wananchi hao wameorodhesha majina na kutia saini fomu, ambayo itapelekwa bungeni kupitia wawakilishi wao.

Tayari wananchi 23,569 katika jimbo la Ubungo, kupitia mbunge wao John Mnyika, wametia saini fomu hiyo.
Serikali imesema kila mwenye kadi ya simu ya mkononi atakatwa sh. 1,000 kwa mwezi, ambapo kwa siku atakatwa sh. 33.35.
Akizungumzia suala hilo jana kwa waandishi wa habari, mjini Dar es Salaam, Mnyika alisema wananchi wanataka taarifa zitolewe kwa umma kuhusu tozo hiyo.
Mnyika alisema wananchi wengi wanataka muswada wa sheria upelekwe bungeni katika mkutano ujao ili kufuta tozo hiyo.
Waziri wa Fedha, Dk. William Mgimwa, akitoa ufafanuzi kuhusu tozo hiyo wiki iliyopita, alisema kila mteja anayemiliki kadi ya simu atakatwa sh. 33.35 kwa siku.
Alisema mapato yote yatakayokusanywa takriban sh. bilioni 160, yatasaidia kuboresha sekta ya nishati na maji.
Kwa mujibu wa serikali, mapato yatakayotokana na tozo hiyo yataharakisha maendeleo katika sekta ya maji, Wakala wa Umeme Vijijini (REA) na Mfuko wa Barabara, kwa ajili ya ujenzi wa barabara za vijiji.
Dk. Mgimwa alisema uamuzi wa kuwalipisha wananchi tozo hiyo ni sahihi, kwa kuwa ni sehemu ya utekelezaji na uharakishaji maendeleo yao.
Alisema kiasi hicho cha fedha ni kidogo, kwa kuwa awali tume ya wataalamu iliyoundwa kutathmini suala hilo ilipendekeza tozo ya sh. 1,450, lakini serikali ikabadili kwa kuwa haipendi kuwaumiza wananchi.
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Fedha, Janet Mbene, alisema mchakato wa tozo hiyo haukuja juu juu, bali ulifanyiwa utafiti, hivyo kuwataka wanasiasa kuacha kuchanganya siasa na uchumi.
Naibu waziri alisema anashangazwa na maneno ya propaganda yanayoenezwa kutoka kwa wanasiasa na kampuni za simu, kwa kuwa hayana mashiko, kwani wanachanganya siasa na utaalamu.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru