Wednesday 17 July 2013

CCM yakataa tozo ya simu


NA MWANDISHI WETU
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimepinga tozo ya sh. 1,000 kwa mwezi kwa kila kadi ya simu.
Taarifa iliyotolewa jana na Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, imesema CCM inapinga tozo hiyo kwa sababu itaongeza mzigo kwa wananchi wa kawaida.
Nape amesema tozo hiyo pia itasababisha usumbufu usiokuwa na sababu kwa wananchi.
Tozo hiyo ilipitishwa na Bunge mwezi uliopita, ikielezwa ni utaratibu wa kawaida wa kuibua vyanzo vipya vya kodi, pale vinapoondoshwa vilivyopo kwa sababu mbalimbali.
Nape alisema licha ya umuhimu wa tozo hiyo, vigezo vilivyotumika kupanga viwango sawia kwa kila mtu mwenye kadi ya simu havijazingatia hali tofauti za kipato kwa Watanzania.
Alisema Watanzania wengi matumizi yao ya simu ni ya kiwango cha chini mno.
“Chama tawala tunaona hatuwezi kukaa kimya kwenye jambo ambalo tunaliona linawabebesha mzigo wananchi, na huenda likarudisha nyuma maendeleo na
kuchelewesha jitihada za kuboresha maisha ya Watanzania kwa jumla,” alisema.
Kutokana na hilo, CCM inaitaka serikali kuangalia njia mbadala ya kukusanya kodi ili kuziba pengo litakalosababishwa na kuondoshwa tozo ya kadi za simu bila kusababisha usumbufu kwa umma.
Utekelezaji wa malipo ya tozo hiyo umeanza Julai mosi, mwaka huu, ambao ndiyo mwezi wa kwanza wa mwaka wa fedha wa  2013/2014.
Katika hatua nyingine,
mbunge wa Musoma Mjini, Vincent Nyerere, alisema anakusanya maoni ya mtu mmoja mmoja kabla ya kufanya mkutano wa hadhara ili kujua wananchi wanataka nini kuhusu tozo hiyo.
Naye mbunge wa Busega, Dk. Titus Kamani, alisema kwa kuwa suala hilo limeshapitishwa na Bunge, hakuna la kufanya.
“Kodi hii itaongeza uwezo wa nchi kuboresha miundombinu na mahitaji ya wananchi vijijini,” alisema.
Selemani Bungara, mbunge wa Kilwa Kusini, kwa upande wake alisema ana wakati mgumu jimboni kutokana na wananchi kutoa maneno ya kashfa kwamba, waliopitisha tozo hiyo wamewaangusha wananchi.
Alisema wananchi hawajaelewa kwa nini wabunge wamepitisha tozo hiyo.
Waziri wa Fedha, Dk. William Mgimwa, akifafanua kuhusu tozo hiyo wiki iliyopita alisema kila mteja anayemiliki kadi ya simu atakatwa sh. 33.35 kwa siku.
Dk. Mgimwa alisema mapato yote yatakayokusanywa takriban sh. bilioni 160, yatasaidia kuboresha sekta ya nishati na maji.
Kwa mujibu wa serikali, mapato yatakayotokana na tozo hiyo yataharakisha maendeleo katika sekta ya maji, Wakala wa Umeme Vijijini (REA) na Mfuko wa Barabara, kwa ajili ya ujenzi wa barabara za vijiji.
Dk. Mgimwa alisema uamuzi wa kuwalipisha wananchi tozo hiyo ni sahihi, kwa kuwa ni sehemu ya utekelezaji na uharakishaji maendeleo yao.
Alisema kiasi hicho cha fedha ni kidogo, kwa kuwa awali tume ya wataalamu iliyoundwa kutathmini suala hilo ilipendekeza tozo ya sh. 1,450, lakini serikali ikabadili kwa kuwa haipendi kuwaumiza wananchi.
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Fedha, Janet Mbene, alisema mchakato wa tozo hiyo haukuja juu juu, bali ulifanyiwa utafiti, hivyo kuwataka wanasiasa kuacha kuchanganya siasa na uchumi.
Naibu waziri alisema anashangazwa na maneno ya propaganda yanayoenezwa kutoka kwa wanasiasa na kampuni za simu, kwa kuwa hayana mashiko, kwani wanachanganya siasa na utaalamu

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru