Friday 19 July 2013

Chenge awajia juu askari Polisi


Chibura Makorongo, Simiyu
MBUNGE wa Bariadi Mashariki mkoani hapa Andrew Chenge, amekemea tabia za baadhi ya askari Polisi kuwanyanyasa madereva wa bodaboda.
Alisema madereva hao wanapaswa kuheshimiwa na inapotokea wanavunja sheria, wanapaswa kuelekezwa na kupewa adhabu stahili badala ya kunyanyaswa ikiwemo kuchapwa viboko.
Kauli hiyo ya Chenge imekuja baada ya kupokea malalamiko ya madereva wa bodaboda waliyoyatoa kwenye mkutano wa hadhara aliokuwa akiuhutubia.
Walidai kuwa huchapwa viboko na Polisi pale wanapowabaini kufanya makosa.
Katika mkutano huo uliohudhuriwa na umati mkubwa wa watu wakiwemo vijana na viongozi wa CCM, madereva hao waliwanyooshea vidole Polisi.
“Naona malalamiko mengi yanaelekezwa  kwa Polisi na bodaboda, sasa suala hili nitalifanyia kazi haraka ili vijana waachwe wafanye kazi, ili wasaidie maendeleo. “Wafanye kazi kwa kuzingatia sheria na ikitoa wamekosea waelezwe si kuwakimbiza huku ni kuwakosesha riziki,” alisema Chenge.
Katika madai yao, madereva hao walisema mara nyingine husababisha ajali kufuatia kukimbizwa na Polisi.
Baadhi yao walidai kuwa huchapwa viboko na askari hao.
Pia, wamedai huombwa kutoa rushwa na kwamba, wamekuwa wakibambikiwa makosa ili wahalalishe rushwa.


Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru