Monday 29 July 2013

Waliotaka kuiibia serikali waumbuka


NA SAMSON CHACHA, TARIME
MAJINA 281 kati ya 1,102 ya wakazi wanaotakiwa kulipwa fidia baada ya nguzo za umeme kupita katika maeneo yao, yamebainika kuwa hewa.
Wakazi hao ni wa kutoka vijiji vya Mogabiri na Itiryo, vilivyoko wilayani Tarime, mkoani Mara.
Imeelezwa pia kati ya majina hayo, 132 ya watu kutoka maeneo mengine yaliingizwa katika orodha ya walipwa fidia kwa lengo la kuihujumu serikali.
Kati ya hayo majina 132 yalikuwa na fomu hewa ambayo yaliingizwa na baadhi ya watu waliokuwa wakitaka kuiibia serikali hivyo hajalipwa fedha kutokana na udanganyifu huo.
Ufisadi huo uliibuliwa na wakazi 200 kutoka katika vijiji 11 ambavyo mradi huo wa umeme unapita.
Walifanya kikao cha dharura na Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo Amos Sagara na Mkurugenzi Mtendaji, Athuman Akalama juzi.
Awali, Halmashauri iliunda Tume ya kuchunguza tatizo hilo, ambapo ilikuja na majibu kama yanayodaiwa na wakazi wa vijiji hivyo, baada ya kufanya uhakiki wa majina na kubaini mengi ni hewa.
“Serikali Kuu ilituletea sh.bilioni 1.5 kwa ajili ya kulipa fidia kwa wale waliotoa maeneo yao kwa ajili ya kupitisha nguzo za umeme kwenda katika vijiji vyenu 11, vikiwemo vya Mogabiri, Nyamwigura, Rosana, Kemakorere, Nyarero, Nyamwaga, Kisangura, Muriba A na Mriba B, Bungurere na Itiryo,” alisema Mkurugenzi mtendaji Akalama.
Hata hivyo, alidai kuwa baada majina yaliyoorodheshwa awali yalikuwa 1,102.
Alisema kabla kazi ya kuanza kulipa fidia, walipeleka majina katika ofisi za vijiji hivyo 11, ambapo yalubandikwa kwenye mbao za matangazo.
Akarama, alisema hatua hiyo iliibua malalamiko kutoka kwa watu mbalimbali kuwa majina yao hayapo.
Mkurugenzi huyo alisema baada ya kupokea malalamiko, walikaa na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya na kuunda tume iliyofanya kazi ya  kuhakiki majina kabla ya kuanza kulipa fidia hiyo.
Alisema tume hiyo iliwashirikisha maofisa usalama wa taifa wilaya, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) na  wa idara ya ardhi.
“Ndipo ilibainika kuwepo kwa majina 281 hewa, majina 132 yalikuwa yana fomu za majina hewa na majina  halali yalikuwa 430,” alisema.
Naye Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo Sagara, alisema serikali hailipi fedha bila kuhakiki na kujiridhisha kwa wanaodai ili haki itendeke kwa pande zote mbili.
Alisema baada ya uhakiki huo, wataanza kulipa Agosti 22, mwaka huu. Hivyo, alitoa wito kwa wote ambao wanastahili kufika bila kukosa.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru