Sunday 28 July 2013

Siasa chafu zatikisa Tarime


na mwandishi wetu
WANACHAMA wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani Tarime, Mara, wameuomba uongozi wa juu wa chama hicho kuwachukulia hatua kali baadhi ya makada wanaofanya kampeni chafu.
Wamesema makada hao wamekuwa wakifanya kampeni chafu zenye lengo la kuwagawa wanachama makundi katika kata mbalimbali kwa lengo la kusaka ubunge mwaka 2015.
Pia, wameonya kuwa hawako tayari kugeuzwa bidhaa ya kisiasa kwani mchezo huo ni hatari kwa mustakabali wa Chama wilayani humo na wameapa kulifikisha suala hilo kwa Katibu Mkuu Abdulrahman Kinana, ili alidhibiti mapema.
Kauli za wanachama hao zimetokana na baadhi ya makada kudaiwa kuanza kampeni za kusaka ubunge katika Jimbo la Tarime, ambapo wengine wamekuwa wakikusanya wajumbe na viongozi kadhaa kufanya vikao vya siri na kupanga mikakati nyakati za usiku.
Jimbo la Tarime kwa linaongozwa na Nyambari Nyangwine, ambaye amekuwa mstari wa mbele katika kutatua kero za wananchi wake ikiwa ni utekelezaji wa Ilani ya CCM na ahadi alizotoa wakati wa kampeni.
Wakizungumza juzi wanachama hao wamesema wamekuwa wakikerwa na kuchukizwa na siasa chafu
zinazoendeshwa na wenzao na kwamba, zisipokomeshwa mapema zinaweza kuleta mpasuko. Wamesema wanatambua kila mwana-CCM ana haki ya kuchagua na kuchaguliwa, lakini hilo ni lazima lifanyike kwa mujibu wa taratibu za Chama na kinyume cha hapo ni usaliti ambao haustahili kufumbiwa macho.
Wamesema mbunge wa sasa (Nyambari), amefanya kazi kubwa katika kuhakikisha Ilani ya CCM inatekelezwa na suala la msingi ni kupewa ushirikiano na fursa ya kutimiza yale aliyoahidi.
“Mwenyekiti wetu taifa, Rais Jakaya Kikwete anasema kila siku tuache siasa chafu na tuwasaidie waliopo madarakani kutekeleza Ilani. Tumechoshwa na hawa wanaotaka kutulaghai kila kukicha wakitaka tuwaunge mkono wakati muda wa kampeni na uchaguzi bado,” alisema Marwa  Nyamhanga.
Alisema kwa muda mrefu CCM ilikuwa na wakati mgumu katika Jimbo la Tarime kutokana na kutawaliwa na upinzani, walijenga umoja na kufanikiwa kulirejesha mikononi ila kuna wachache wanataka kuleta mpasuko.
Naye Masero Mroni alisema, aliwatuhumu baadhi ya makada wa CCM walioshindwa kwenye mchakato wa kura za maoni na Nyangwine, ambao sasa ndio wameanza kuleta chokochoko na kuwagawa wanachama.
Hata hivyo, alisema kuwa kamwe hawatakubali kuingizwa kwenye siasa chafu kwa maslahi ya watu wachache na kwamba, watasimama imara kwa maslahi ya CCM na si vinginevyo.
Pia, alimtuhumuwa mkuu wa wilaya (jina linahifadhiwa) kuwa ni miongoni mwa chanzo cha kuleta mpasuko na makundi kwa wana-CCM.
Alisema kiongozi huyo amekuwa akiwarubuni wanachama kujiunga na kambi yake kwa madai kuwa ana uhakika mwaka 2015 ubunge ni wake, jambo ambalo kwa sasa halikubaliki kwa kuwa Chama bado kina viongozi wanaoendelea na kazi.
Kwa upande wake, Bhoke Mwita, alisema kwa wanachama kukubali kuanzisha makundi ni usaliti kwani, utaratibu wa Chama ni kumsaidia aliyepo madarakani kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM.
Bhoke alitumia fursa hiyo kumuomba Katibu Mkuu wa CCM, Kinana kuingilia kati na kuwaonya wale wote wanaojaribu kuvuruga utaratibu wa Chama.
“CCM ina wenyewe na ndio sisi, kitendo cha watu wachache kutaka kutuvuruga na kutugawa ni kuandaa mazingira ya kurejesha jimbo kwa upinzani na hilo hatutalikubali. Namuomba Mheshimiwa Kinana awaadhibu hawa wenzetu ili tuendeleza umoja na mshikamano wetu,” alisema Bhoke.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru