Friday 19 July 2013

Mama Salma akemea ubaguzi


Na Anna Nkinda, Maelezo
MKE wa Rais, Mama Salma Kikwete, amewataka wanawake kutobaguana kutokana na itikadi za kisiasa au dini, badala yake wawe mstari wa mbele kuhubiri amani na upendo.
Alisema hayo jana wakati wa futari aliyowaandalia wanawake Ikulu, jijini Dar es Salaam.
Mama Salma alisema ukosefu wa amani ukitokea katika nchi wanawake na watoto ndio waathirika wakubwa, hivyo wasikubali kudanganywa.

Amewataka kuwa na msimamo ili kuilinda amani, ambayo ni silaha ya ukombozi.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Jumuia ya Wanawake wa Kiislamu Tanzania, Shamim Khan, alimshukuru Mama Salma kwa upendo wake.
Shamim alisema kukutana kwao kumewafanya wajifunze kuwa, wakitaka amani ni lazima washirikiane bila kujali rangi, dini au kabila, kwani wanawake wote wana matatizo yanayofanana, ambayo wanaweza kuyatatua kwa pamoja.
Naye Olive Lwema, ambaye ni Mwenyekiti wa Jumuia ya Wanawake Wakristo Tanzania, alisema wamefurahishwa na mwaliko wa Mama Salma.
Alisema wanapokutana wanawake, ambao ni wazazi wa watoto wa taifa na wake wa wanaume wanaoongoza nchi, hakuna jambo litakaloharibika.
Olive aliwaomba wanawake wanaofunga katika kipindi hiki cha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani, wajitoe kwa ajili ya kuomba amani.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru