Monday 15 July 2013

Red Brigade’ ni magenge ya kigaidi, utekaji nyara, utesaji, uuzaji wa dawa za kulevya na umwagaji damu


CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimetangaza rasmi kuanzisha kambi za kijeshi nchini kote ili kuwapa mbinu za kivita vijana wake wanaoitwa “Red Brigade”, kazi ambayo hata hivyo ilishaanza siku nyingi.

Katika kufanya hivyo, Mwenyekiti wa Taifa wa Chadema, Freeman Mbowe aliwaambia waandishi wa habari hivi karibuni kuwa chama chake kimechukua hatua hiyo baada ya serikali na vyombo vyake vya ulinzi na usalama, kushindwa kuyafanyia kazi malalamiko yao kuhusu mauaji, vitisho na matukio na kutisha wanayofanyiwa baadhi ya viongozi na wanachama wao.
Siku moja baadaye, chama hicho kililisusia Kongamano la Amani lilloiandaliwa na Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD) jijini Dar es Salaam na mgeni wake rasmi kuwa Rais Jakaya Kikwete, yule ambaye katika hotuba yake ya ufunguzi alishangaa kitendo hicho cha Chadema na kuhoji:
“Hawa kweli wanapenda amani yetu wakati hawapendi tuzungumze? (Ina maana wao) wanataka watu wauane au wapigane?”
Alipokuwa akiongea na waandishi wa habari katika Makao Makuu ya Chadema yaliyopo Mtaa wa Ufipa, Kinondoni jijini Dar es Salaam, Ijumaa iliyopita, Mkurugenzi wa Mafunzo na Organaizesheni wa Taifa wa Chadema, Benson Kigaila alisisitiza kuwa mafunzo hayo hayatasitishwa ila yataendelea ingawa tayari yameshapigwa marufuku na polisi nchini.
Akizungumzia suala hilo Alhamisi iliyopita, Msemaji wa Jeshi la Polisi Tanzania, Advera Senso alisema hatua yoyote ile chama chochote cha siasa kuanzisha kikundi cha kujihami ni kinyume cha sheria, hivyo kama Chadema haitasitisha nia yake hiyo itachukuliwa hatua mara moja.
“Kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni haki ya raia yeyote kujilinda. Chadema ni taasisi (na hivyo) ni haki yetu kuilinda na ndiyo maana tumesajili kikundi chetu cha ulinzi.
“Sasa nani anatutisha? Tunataka polisi waanze na CCM kwanza ambao katika mafunzo yao wanafundisha hadi kupiga saluti na kutumia silaha”, alisema Kigaila ambaye kwa wanaoifahamu hulka yake wanajua jinsi anavyopenda shari muda wote.
Ndiyo maana alishiriki kutaka kumpindua Mwenyekiti wa Taifa wa Chama cha United Democratic (UDP), John Momose Cheyo mwaka 2003 na kujikuta akifukuzwa uanachama na uongozi aliokuwa nao huko na kukimbilia Chadema.
Alidai kuwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kiliweka makambi yenye jumla ya vijana 800 katika mikoa ya Shinyanga, Singida na Tabora ambao baadaye walipelekwa Igunga wakati wa uchaguzi mdogo wa ubunge wa jimbo hilo mwaka 2011 na kusababisha kifo cha kada mmoja wa Chadema, Msafiri Mbwambo.
Alidai hata mwaka jana, CCM iliandaa mafunzo ya kitaifa kwa vijana wake wanaoitwa Green Guard huko Mwanza, yale ambayo yalihitimishwa kwa gwaride lililokaguliwa na Mwenyekiti wa Taifa wa Chama hicho, Jakaya Kikwete; Makamu Mwenyekiti (Tanzania Bara), Philip Mangula na Katibu Mkuu, Abdulrahman Kinana.
Sipendi kuamini uongo na hata uzushi kwa vile sipendi kabisa kuwadanganya wananchi na hata vinginevyo.
Vijana wa Green Guard ambao wanatoka katika Idara ya Chipukizi na Uhamasishaji ya Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) siyo wanajeshi, mgambo na wala hawana kabisa mbinu za kijeshi kama alivyodai Kigaila na kamwe kazi zao siyo za kivita.
Mafunzo makubwa wanayopewa wanapokwenda kambini ni ujasiriamali kikiwemo kilimo cha mashamba makubwa, kilimo cha umwagiliaji kama vile bustani, ufugaji wa nyuki, kazi za mikono na kujitolea, uvuvi, uvumilivu, mapokezi ya viongozi wa chama chao na maisha ya kijamaa.
Wanapata mafunzo hayo kwa kutumia mapanga, shoka na majembe kwa kilimo na kufyeka misitu kwa ajili ya kilimo na maandalizi ya mashamba, nyavu za kuvulia samaki, mbao zilizotengenezwa kama bunduki kwa ajili ya kufanyia mazoezi ya gwaride la kuwapokelea viongozi wa chama chao, zile ambazo hata hivyo wanapokuwa wakiwapokea hawazitumii popote wala silaha yoyote.
Hawapigi saluti yoyote ile ya kijeshi kama alivyodai Kigaila isipokuwa za mfumo wa aina yake na salaam tu maalum kwa ajili ya viongozi waandamizi wa chama chao, jambo ambalo halina ubaya wowote isipokuwa linapotoshwa ili kutaka kuhalalisha malengo ya kigaidi ya Red Brigade!
Hata kambi hizo zenyewe hazifanyiki mijini isipokuwa vijijini kwenye mashamba, mifugo, mabwawa ya ufugaji au yenye samaki, mizinga ya kufugia nyuki, bustani za kuku na kazi nyingine za kijasiriamali.
Anayetaka kujua ukweli huu aende katika Chuo cha Itikadi cha Ihemi kilichopo wilayani Iringa ili akayaone mashamba makubwa kabisa ambayo yapo mahali hapo. Atajionea namna vijana hao wa CCM wanavyofundishwa kazi za mikono, kilimo cha bustani na mashamba makubwa, uvumilivu pamoja na upendo kwa kila mtu.
Kana kwamba haitoshi, CCM kamwe haina kabisa mfumo wa gwaride moja la chipukizi wake au vijana wa Green Guard kukaguliwa wakati mmoja na zaidi ya kiongozi wake mmoja isipokuwa vinginevyo.
Haina utaratibu wa ovyo wa Kichadema wa viongozi wake wakuu kama Mwenyekiti wa Taifa, Makamu Mwenyekiti na Katibu Mkuu kufuatana pamoja katika tukio moja.
Hata tarehe 5 Februari ya kila mwaka hawafuatani pamoja kwenye sherehe  zake isipokuwa hukutania uwanjani na hatimaye hutawanyika kila mmoja kwa muda wake, halafu hawafanyi kabisa kazi zinazofanana ila kila kiongozi anakuwa na jukumu lake na kuzingatia itifaki.
Mafunzo yanayotolewa kwa vijana wa Chadema ambayo kwanza yalishaanza siku nyingi katika baadhi ya mikoa kama Shinyanga ni mbinu za kijeshi, mapigano ya kivita zikiwemo kung-fu, utumiaji wa silaha hususan mapanga, visu vya kurusha, fimbo na kadhalika.
Ndivyo ilivyokuwa kwenye viwanja vya Shule ya Sekondari ya Mazinge iliyopo kata ya Ndembezi na baadhi ya maeneo ya Ibinzamata, Kizumbi na Ngokolo mjini Shinyanga.
Wamekuwa wakifundishwa hasa nyakati za jioni hadi usiku kwa kubadili mafunzo kadri muda unavyokwenda ambapo mchana huanza kama watu wanaofanya mazoezi ya kawaida ya viungo, halafu usiku ndipo wanafundishwa mbinu za kijeshi wakianza na nadharia na hatimaye vitendo.
Mbowe na Kigaila wanapodai eti chama chao ndiyo kwanza kinataka kiwafundishe vijana wake mafunzo ya kuwalinda viongozi na wanachama wao wanadanganya waziwazi na bila aibu japokuwa kidogo!
Wanajua kuwa vijana kutoka nje ya mkoa wa Shinyanga ndio waliokuja kuwafundisha Red Brigade wao mbinu za kigaidi, na kwamba wanapodai hayo eti ni mafunzo ya kujilinda ama kuwalinda viongozi na wanachama wao wanasema uongo.
Hivi viongozi wa Chadema kama Katibu Mkuu, Dk. Wilbroad Slaa au Wajumbe wa Kamati Kuu akina Zitto Kabwe, Godbless Lema, Peter Msigwa, John Mnyika, John Heche, Tundu Lissu na kadhalika wawe wanalindwa na vijana wa Red Brigade dhidi ya nani au kwa kitu gani walichonacho?
Kama hata viongozi waandamizi wa serikali kama vile Mawaziri, Naibu Mawaziri, Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya au Makatibu Wakuu wa Wizara, Wakurugenzi Watendaji wa Halmashauri za Majiji, Manispaa, Miji au Wilaya ambao kuna wakati hutoa maamuzi mazito yanayohusu mpaka maisha ya watu wengine hawana ulinzi; hawa wa Chadema wana nini?
Mbali na hayo, kudai eti kazi kubwa ya kikosi cha Red Brigade ni kuwalinda viongozi na wanachama wa Chadema kutokana na tishio lolote lile ni uongo na uzushi.
Nafahamu kwamba kinachofanywa na chama hicho ni kuibua visingizio vya kutaka shari kila kunapokucha ili kutafuta mbinu au mikakati ya kuendeleza vurugu zao, kusimamisha majukumu ya serikali zikiwemo kazi za kushughulikia maendeleo ya wananchi na badala yake ibaki ikihangaikia malumbano yasiyokuwa na tija yoyote kwa taifa letu.
Nawashangaa Mbowe na Kigaila wanapodai kuwa Chadema imeamua kutoa mafunzo hayo kwa Red Brigade wake baada ya serikali na vyombo vyake ya ulinzi na usalama kushindwa kuyashughulikia madai yao ya mauaji, vitisho na matukio mengine ya kutisha yanayofanywa dhidi ya wanachama na viongozi wao.
Rekodi ya mauaji yatokanayo na harakati mbalimbali za vyama vya siasa nchini yamekuwa yakisababishwa kwa kiwango kikubwa zaidi na Chadema yenyewe, hivyo haiwezekani kuja kuisingizia serikali au vyombo vya ulinzi na usalama kwamba haviwasikilizi wanapokwenda kulalamikia suala hilo.
Mathalani, vurugu zilizoacha mauaji ya wananchi watatu yaliyotokea Januari 5, 2011 mjini Arusha zilisababishwa na viongozi wa Chadema ambao ni pamoja na Mbowe binafsi, Dk. Slaa, Kigaila pamoja na wabunge takribani wote wanaotoka chama hicho na kadhalika.
Wote walishirikiana kwa jeuri, kejeli, kebehi na dharau kwa kukaidi ushauri wote waliopewa kwa kuelimishwa, kuonywa na hata kubembelezwa kwamba wasifanye maandamano wakati wa kwenda kwenye mkutano wao uliokuwa ufanyike mjini humo.
Kilichotisha zaidi ni kuandamana kwa ghasia, vurugu au fujo kwa kupita barabarani, mitaani na maeneo mbalimbali ya jiji hilo huku wakipiga watu, kuchoma nyumba, magari, ofisi ama maduka na vibanda vya wafanyabiashara waliokuwa wakiwashutumu kwamba hawawaungi mkono na kuwa upande wa serikali, CCM au Jeshi la Polisi.
Walikuwa wakiandamana huku wakimwaga kila aina ya matusi yakiwemo yale ya nguoni, kuwatisha au kuwashambulia watu bila hatia yoyote au kuwakejeli kwa maneno machafu mpaka viongozi waandamizi wa serikali ya nchi yetu!
Kibaya kinachotisha zaidi ni pale walipobadili mwelekeo wa kwenda mkutanoni na kutaka kwenda kukiteka kituo Kituo Kikuu cha Polisi cha Mkoa huo ili wakaibe silaha zilizokuwa ndani zikiwemo za kivita, wawatoroshe mahabusu wa makosa mbalimbali waliokuwemo, wawakamate askari wake na hatimaye wakichome moto ili kisiwepo kabisa!
Licha ya kuonywa kwa zaidi ya mara tatu wakitangaziwa kwa kipaza sauti kwamba watawanyike mara moja, wafuasi hao wa Chadema waliotiwa jeuri na viongozi wao waliendelea kukisogelea kituo hicho muhimu kwa usalama wa maisha ya wananchi na mali zao huku wakirusha mawe na kubeba hadi mapanga, sime pamoja na silaha nyingine.
Ni kutokana na hali hiyo ndipo Jeshi la Polisi lilipolazimika kufyatua risasi za moto zilizoua watatu kati yao huku wengine wakijeruhiwa kwa viwango tofauti, hatua iliyopelekea kituo hicho kinusurike kuteketezwa kwa mikakati ya kigaidi.
Mbali na tukio la Arusha, vurugu za Chadema pia zilisababisha kada mmoja wa CCM katika kata ya Ndago huko Iramba, Singida naye apoteze maisha yake na hatimaye mauaji mengine huko Msamvu mjini Morogoro na kijiji cha Nyororo wilayani Mufindi, Iringa.
Wafuasi hao wa Chadema wanatuhumiwa kwenda kumshambulia kada huyo wa CCM kwa silaha za jadi akiwa ndani ya nyumba alimokimbilia ili kunusuru maisha yake, halafu mauaji ya Msamvu na Nyororo yalitokana na ukaidi wa viongozi wa chama hicho kwa vyombo vya dola hasa Jeshi la Polisi nchini.
Wanataka wanapofanya mikutano yao ya hadhara ni lazima waende kwa maandamano hata kama hali na mazingira ya usalama hayaruhusu.
Wakiwa bado Morogoro, serikali ilisitisha kwa muda wa siku saba mikusanyiko yoyote ya kisiasa ikiwemo mikutano ya hadhara ili kupisha zoezi muhimu la sensa na makazi ya watu, lakini viongozi hao wa Chadema walikaidi huku Dk. Slaa akimwandikia ujumbe mfupi wa maneno ya kejeli Inspekta Jenerali wa Jeshi la Polisi Tanzania, Saidi Mwema akimwambia kuwa apeleke askari wa kwenda kupambana naye Iringa!
Aidha, kurushwa kwa bomu lililoua watu watatu wengine siku ya mwisho ya kampeni za Chadema katika Viwanja vya Soweto jijini Arusha hivi karibuni, kuna kila viashiria kwa chama hicho chenyewe kuwa pia kilihusika nalo kwa namna moja ama nyingine.
Haiwezekani kuwa hata baada ya bomu hilo kurushwa na kuibua taharuki nzito mkutanoni, mpigapicha za video iliyodaiwa na Mbowe na Lema kwamba wanayo nakala yake aendelee kuifanya kazi hiyo na bila wasiwasi.
Haiwezekani kabisa Mbowe na Lema eti wasikimbie au kutoroshwa kwa kuyahofia maisha yao, badala yake wakabaki wamesimama kwa utulivu hatua chache tu kutoka lilipolipukia bomu lile huku wananchi wengine wakikimbia ovyo kwa taharuki na baadhi yao wakiangua kilio cha kujeruhiwa kwa viwango tofauti.
Huo ndio ukweli wa vurugu zote za Chadema zinazotokea nchini ambazo hatimaye hivi leo wanataka kuzitumia kwa kutengeneza kikosi cha kigaidi.
Tofauti na jinsi alivyodanganya Kigaila aliposema kuwa “kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni haki kwa raia yeyote kujilinda”, hakuna kifungu hicho popote katika ibara zote za Katiba ya nchi hii.
Tofauti na upotoshaji wake huo, Ibara ya 14 ya Katiba hiyo inasema: “Kila mtu anayo haki ya kuishi na kupata kutoka katika jamii hifadhi ya maisha yake, kwa mujibu wa sheria”.
Mbali na hiyo, Ibara ya 16(2) ya Katiba ileile inasema: “Kwa madhumuni ya kuhifadhi haki ya mtu kwa mujibu wa ibara hii, Mamlaka ya Nchi itaweka utaratibu wa sheria kuhusu hali, namna na kiasi ambacho haki ya mtu ya faragha na ya usalama wa nafsi yake, mali yake na maskani yake yaweza kuingiliwa bila ya kuathiri ibara hii”.
Wapi panaposema “ni haki ya raia yeyote kujilinda” kama inavyopotoshwa na Kigaila? Ni ibara gani ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoruhusu taasisi au kikundi chochote cha watu vikiwemo vyama vya siasa kama Chadema kuanzisha jeshi ama kikosi cha ulinzi?
Ni sehemu gani katika mamlaka halali za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambako Red Brigade ya Chadema imesajiliwa kama kikosi au hata kikundi cha ulinzi kati ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi ama Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa?
Kinyume kabisa cha uongo aliousema Kigaila ambaye namjua kwa miaka mingi kuwa ni mmoja kati ya wazushi mahiri kabisa hapa nchini, Ibara ya 147(1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano nayo inasema ifuatavyo:
“Ni marufuku kwa mtu yeyote au shirika lolote au kikundi chochote cha watu, isipokuwa serikali kuunda au kuweka Tanzania jeshi la aina yoyote”, halafu Kifungu Kidogo cha (2) kinaongeza:
“Serikali ya Jamhuri ya Muungano yaweza, kwa mujibu wa sheria, kuunda na kuweka Tanzania majeshi ya aina mbalimbali kwa ajili ya ulinzi na usalama wa nchi na wananchi wa Tanzania” (mwisho wa kunukuu).
Huo ndio ukweli ambao viongozi wa Chadema wanautengenezea uongo ili kuhalalisha uovu wao kwa nchi yetu. Huo ndio ukweli ambao wanajitahidi sana kuuficha kwa kuwadanyanga Watanzania ili kukidhi matakwa yao ya kigaidi kwa nchi hii.
Mbali na ukweli huo wote, hakuna jeshi lolote duniani lenye Red Brigade (au Brigedi Nyekundu) liwe la mgambo na hata la ulinzi. Kila jeshi la serikali yoyote lina brigedi zake zenye majina yasiyokuwa ya vitisho ama ya shari kama kikosi cha kigaidi cha Chadema.
Mfano katika Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) ambalo mimi nimewahi kuwa afisa wake lina brigedi zenye majina ya Tembo, Chui, Twiga, Faru, Mbuni, Nyuki na kadhalika kama ishara ya kuonyesha utajiri wa asili tulionao nchini. Red Brigade au Brigedi Nyekundu inaashiria shari na vitendo vya kikatili.
Hilo ndilo jina la genge lililotikisa Italia miaka iliyopita likiongoza kwa matukio ya kigaidi ambayo ni pamoja na kuwateka nyara viongozi wa dini na serikali ya nchi hiyo, utesaji wa aina zote, uchinjaji na umwagaji mwingine wa damu ili kuilinda na kuihami biashara yake ya madawa ya kulevya huku pia likiitwa Red Brigade kama ya Chadema!
Huo ndio ukweli ambao mtu yeyote anayetaka ni hivyo na hata asiyetaka pia ni hivyohivyo.

Mungu Ibariki Tanzania!
Mwandishi wa makala hii ni Katibu wa CCM wa Wilaya ya Shinyanga Mjini.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru