Monday 29 July 2013

Mbunge atoa angalizo kwa wana-Mtwara


Na mwandishi wetu
WAKAZI mkoani Mtwara, wameonya kutokubali kuuza ardhi kwa wawekezaji wanaoendelea kuingia kwa kasi mkoani humo.
Alisema hiyo itawasaidia kuepuka kuja kugeuzwa ‘watumwa’ ndani ya mkoa wao, badala yake, waiendeleze wenyewe.
Wito huo ulitolewa juzi jioni na Mbunge wa Tandahimba Juma Njwayo, alipokuwa akihutubia katika mkutano wa hadhara jimboni humo.
Njwayo, yupo jimboni humo kukagua shughuli za maendeleo.
Alisema wimbi la wawekezaji kununua mashamba makubwa na madogo mkoani humo, linaweza kuwa na madhara makubwa baadaye.
Mbunge huyo, alisema Mtwara una fursa nyingi za kiuchumi ambazo zimeanza kuwavutia wawekezaji kutoka maeneo mbalimbali ndani na nje ya nchi.
Katika ziara hiyo, Njwayo alitembelea kata zote 14 zinazounda jimbo hilo na kufanya mikutano ya hadhara, iliyohusisha pia kupokea kero za wakazi hao pia kusaidia harakati za wapigakura wake kujiletea maendelo.
“Kataeni kuuza ardhi, ndio mkombozi Wenu wa baadaye. Wawekezaji wengi wanakimbilia mikoa ya Kusini kwa sasa kutokana na fursa za kiuchumi zinazoendelea kujitokeza,” alisema Njwayo.
Lakini pia aliwatahadharisha kuwa makini na madalali wanaotumiwa na wawekezaji hao kuska ardhi.
Wakati huo huo; aliwaeleza waazi hao kuwa serikali imeanza kuweka umeme kwa awamu ya pili ya 2013-2014, katika vijiji vilivyosalia.
Aliwataka wakazi wa Tandahimba, kujipanga kwa ajili ya kutumia fursa hiyo ya kuwekewa nishati hiyo muhimu kwa maendeleo.
Njwayo alisema vijiji vitakavyokuwa kwenye mpango wa kupata umeme ni Namikupa, Maundo, Nawahonga, Mtikila, Mnyawa, Mahena, Binembo, Mikunda, Lubangala na Mahuta.
Alisema njia nyingine ya umeme itafungwa Tandahimba hadi Mbarala, Lyenje hadi Mkoanjoano, Luagala hadi Itehu na Madaba mpaka Kitama.
Katika ziara hiyo, Njwayo alichangia zaidi ya sh. milioni 14 kwa ajili ya kusaidia miradi mbalimbali ya maendeleo na huduma za jamii.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru